Mar 08, 2026 at 03:55PM
MVUVI mmoja alifariki na mwingine kujeruhiwa vibaya walipopigwa na radi wakivua samaki baharini katika eneo la Ingini, Lamu Jumamosi.
Kassim Badi Usama, 48, alifariki papo hapo ilhali mwenzake, Mohamed Wako, akiachwa na majeraha mabaya baada ya radi kuwachapa walipokuwa kwenye mashua yao wakivua huku mvua kubwa ikinyesha.
Kamanda wa Polisi kaunti ya Lamu, Bw Shadrack Ruto alithibitisha kisa hicho akisema mashua ya wavuvi hao, iliharibiwa kwa kupasuliwa na radi.
Bw Ruto aliwaomba wavuvi kuwa waangalifu na kupunguza shughuli zao baharini msimu huu wa mvua kubwa.
Meneja wa Kitengo cha Majanga na Uokozi (EOC Lamu Iftakkar Majid aliwasisitizia wavuvi, mabaharia na wakazi kuwa waangalifu msimu huu wa mvua kubwa ili kuepuka majanga zaidi.
Bw Majid aliwasihi kutafuta ushauri kutoka kwa kituo hicho cha majanga na pia idara ya hali ya hewa kabla ya kutekeleza shughuli zozote baharini.
“Pia ninawashauri wananchi kutotafuta hifadhi chini ya miti wakati kukinyesha kwani hilo huwaweka kwenye hatari ya kupigwa na radi,” akasema Bw Majid.
Wakati huo huo, familia ya mwendazake, inaiomba serikali kuwapa msaada kutokana na kuondokewa kwa mpendwa wao waliyemtaja kuwa tegemeo la kipekee.
Binamuye mwendazake, Bw Badi Nassir, alisema kakake ameacha mjane na watoto wawili.
“Binamu yangu ndiye tegemeo la familia yake. Mke na watoto wameachwa ukiwa. Serikali izingatie kuifidia familia ili angalau ijitegemee,” akasema Bw Nassir.
Mwenyekiti wa zamani wa Muungano wa Wavuvi (BMU) eneo la Faza ambako marehemu anatoka, Bw Mohamed Ali aliomba fedha za majanga zinazotengwa kila kukicha na serikali pia kuhakikisha zinawafikia wavuvi wa Lamu wanaokumbwa na majanga.
Mar 08, 2026 at 03:33PM
BB BREAD Jumapili, Machi 8, 2026 iliwaangushia ‘Goliath’ Gor Mahia kipigo cha 1-0 uwanja wa Kitaifa wa Nyayo na kufuzu raundi ya 16 ya Kombe la MozzartBet.
Mnamo Februari 10, timu hiyo ilibandua AFC Leopards kupitia mkwaju wa penalti na kufuzu raundi ya 32 kutoka ile ya 64.
Denis Cheni ambaye pia alifunga dhidi ya AFC Leopards ndiye jana alicheka na nyavu za Gor Mahia na kuwabandua kwenye MozzartBet.
“Tulijua tutakutana na timu kubwa na kocha amefanya tujiamini sana kwa sababu mbinu ni zake. Baada ya kutoa Gor na AFC, sasa sisi tunaona tukifika katika fainali,” akasema Chieni.
Kocha wa timu hiyo ni Azastine Okoba.
BB Bread inayoshiriki Ligi ya Shirikisho la Soka Nchini (FKF) Nairobi Magharibi sasa ni kati ya timu zinazoshiriki ligi za chini ambazo zimesalia katika mashindano hayo.
Hii ina maana kuwa Gor wamebanduliwa Kombe la MozzartBet na sasa nafasi yao ya mechi za CAF ni kushinda ubingwa wa Ligi Kuu Nchini (KPL).
Kando na masaibu ya Gor, timu nyingine zinazoshiriki KPL nazo ziliendelea kutamba dhidi ya wapinzani kutoka ligi za chini.
Mabingwa watetezi Nairobi United waliweka hai matumaini yao ya kuhifadhi taji hilo, wakiwashinda BMC All Stars 8-0 uwanja wa Ulinzi Sports Complex.
Mvamizi Benson Omala, Ashraf Thaire na Benard Magare waliyafunga mabao mawili kila moja huku Duncan Omala na Shami Kibwana wakiongeza mengine.
Humprey Aroko naye alifunga mabao manne na kusaidia Kariobangi Sharks kuwachapa KU Hardnuts 4-0 uwanja wa Kasarani.
Mabingwa wa 2023 Kakamega Homeboyz nao walishinda Kipchimchim FC 3-0 huku Oliver Majak akifunga mabao mawili na Eston Omengo akiongeza jingine uwanja wa Bukhungu.
Dinken Mwema alifungia Posta Rangers magoli mawili Oinopsos 2-0 uwanja wa Afraha Kaunti ya Nakuru.
Chebaiywa Lions nao waliwapiga Gucha Youth 2-0 uwanja wa DMI St Joseph's Science School, Eldoret nao.
Murangá Seal walifunga Dynamo FC 1-0 uga wa SportPesa Arena kupitia goli la Victor Haki kipindi cha kwanza.
Mar 08, 2026 at 02:04PM
CHELSEA na Machester City, walijiunga na Arsenal kufuzu robo fainali ya Kombe la Michuano ya FA Jumamosi usiku.
The Blues walitoka nyuma mara mbili na mwishowe wakapata ushindi wa 4-2 dhidi ya Wrexham ya Wales nao City wakawanyorosha wenzao wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) Newcastle 3-1.
Ilikuwa mechi yenye presha nyingi huku Sam Smith akifungia Wrexham bao la kwanza dakika ya 18 kwa kuutumia vizuri udhaifu wa safu ya ulinzi ya Chelsea.
Lakini wing'a Alejandro Garnacho alilazimisha bao la kujifunga kabla ya mapumziko wakati juhudi zake za kufunga, zilipoondolewa na beki George Thomason na kumpiga mlinda mlango wa Wrexham, Arthur Okonkwo, mgongoni na mpira ukaingia wavuni.
Katika kipindi cha pili, Chelsea ilifanya mabadiliko kadhaa baada ya dakika 45 mbovu, lakini Wrexham walipata tena bao la uongozi dakika ya 78 kupitia Callum Doyle.
Dakika nne baadaye, Chelsea walisawazisha kwa mara nyingine kupitia Josh Acheampong na mechi hiyo ikaishia sare 2-2 na kuelekea muda wa ziada.
Wenyeji hao walipata pigo dakika ya (90+3) wakati George Dobson alipata kadi nyekundu.
Mechi iliendelea hadi dakika za ziada na kombora la Alejandro Garnacho katika muda wa ziada ambalo liliwaweka mbele kwa mara ya kwanza, huku mchezaji wa akiba Joao Pedro akifunga bao la nne.
Chelsea watacheza ugenini dhidi ya PSG Jumatano hii katika hatua ya 16 bora ya Ligi ya Mabingwa.
Katika mechi Ugani St James' Park, mabao ya Savinho (39), Omar Marmoush na (47, 65) yalitosha kuipa City ushindi dhidi ya Newcastle ambao walipata bao la kufutia machozi kupitia Harvey Barnes (18).
Baada ya mechi hii, Newcastle watakabiliana na Barcelona katika mechi ya kwanza ya hatua ya 16 bora ya Ligi ya Mabingwa katika uwanja wa St James' Park siku ya Jumanne, kabla ya kusafiri hadi Stamford Bridge.
City nao watasafiri hadi Santiago Bernabeu kuwakabili Real Madrid katika mechi ya kwanza ya hatua ya mwondoano ya Ligi ya Mabingwa Jumatano, kabla ya kucheza na West Ham katika uwanja wa London siku ya Jumamosi mechi ya EPL.
Baadae leo, West Ham itakuwa mwenyeji wa Brentford katika mechi nyingine ya FA.
Mar 08, 2026 at 12:48PM
BEIRUT/MIAMI/TEL AVIV/DUBAI
RAIS Donald Trump amesema hana nia ya kujadiliana na Iran, na kuzua uwezekano kwamba vita vya Iran vitaisha tu wakati jeshi na uongozi wa Tehran utakapoangamizwa kabisa.
Muda mfupi baada ya Trump kuzungumza na wanahabari ndani ya ndege rasmi ya Rais, Air Force One, Israel, mwandani wa Amerika, ilitangaza mashambulizi mapya kote nchini Iran mapema Jumapili, huku vita hivyo ambavyo vimesababisha hisia kali Mashariki ya Kati na kuvuruga masoko ya mafuta duniani vikiingia wiki ya pili.
“Wakati fulani, sidhani kutakuwa na mtu yeyote wa kusema, ‘tumesalimu amri’,” alisema Trump.
Trump ametetea operesheni kubwa zaidi ya kijeshi ya Amerika katika ukanda wa Mashariki ya Kati tangu uvamizi wa 2003 nchini Iraq, akisema Tehran ilikuwa tishio kwa Amerika pasipo kutoa ushahidi.
Amesema vilevile Iran ilikuwa karibu mno kufaulu kujenga silaha ya kinuklia.
Amerika na Israel zimejadiliana kuhusu kutuma vikosi maalum nchini Iran kutwaa madini yake ya uranium katika hatua za mwisho za vita, shirika la Axios liliripoti, likinukuu watu wanne wanaofahamu majadiliano hayo.
Alipoulizwa Jumamosi kuhusu uwezekano wa kutuma vikosi vya jeshi la ardhi kutwaa vituo vya nuklia, Trump alisema ni jambo wanaloweza kufanya “baadaye”.
[caption id="attachment_185544" align="alignnone" width="1080"] Mojtaba Khamenei, mwanawe Ayatollah Khamenei anayepigiwa upatu kumrithi mkuu huyo aliyeuawa kwenye shambulio la Amerika-Israel dhidi ya Iran Februari 28, 2026. Picha|Hisani[/caption]
Serikali za Saudi Arabia, Kuwait, Milki ya Kiarabu, na Bahrain ziliripoti mashambulizi ya droni yaliyotekelezwa na Iran katika mataifa yao Jumamosi na mapema Jumapili, huku moto mkubwa ukiteketeza jengo la afisi za serikali jijini Kuwait.
Ubalozi wa Amerika katika jiji kuu la Norway, Oslo, vilevile lilishambuliwa na mlipuko Jumapili na kusababisha uharibifu kiasi pasipo majeraha yoyote, polisi walisema.
Haikubainika papo hapo ni nini kilichosababisha mlipuko na nani alihusika.
Saudi Arabia imeambia Tehran kuwa mashambulizi yanayoendelea kutekelezwa na Iran dhidi ya milki hiyo huenda yakaisukuma Riyadh kulipiza kisasi, watu wanaofahamu suala hilo walieleza Reuters.
Kwenye jaribio la kutuliza hamaki kote eneo la Ghuba, Rais wa Iran, Masoud Pezeshkian aliomba radhi nchi jirani kwa mashambulizi yake dhidi ya vituo vya Amerika katika mataifa hayo Jumamosi.
Alipuuzilia mbali matakwa ya awali ya Trump akiitaka Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kujisalimisha kama “ndoto” lakini akasema baraza la uongozi limekubali kusitisha mashambulizi kwa nchi jirani isipokuwa pale mashambulizi dhidi ya Irani yanapotoka maeneo yao.
Matamshi ya Pezeshkian yalizua hisia mseto nchini Iran na kuilazimu afisi yake kusisitiza Iran itajibu vikali mashambulizi kutoka ngome za Amerika.
Kundi la kidini lililotwikwa jukumu la kumchagua kiongozi mpya wa kiroho Iran, kumrithi Ayatollah Ali Khamenei, aliyeuawa kwenye shambulizi wiki iliyopita lilitazamiwa kukutana Machi 8, 2026, vyombo vya habari Iran vilisema.
Sehemu kubwa ya wanachama imeafikiana kuhusu mrithi, alisema mwanachama wa Baraza la Wataalamu, Ayatollah Mohammadmehdi Mirbaqeri, kulingana na shirika la habari la Mehr.
Duru zilieleza awali kuwa huenda Mojtaba Khamenei akachaguliwa na baraza hilo la wanachama 88 kumrithi Ali Khamenei.
Milipuko mikubwa ilisikika katika sehemu za Tehran, vyombo vya habari vilisema, huku Israel ikisema ilishambulia vituo vya makombora, vituo vikuu vya kuamuru mashambulizi na vya mafuta Jumamosi.
Mashambulizi ya Amerika–Israel yamewaua raia wa Iran wasiopungua 1,332 na kuwajeruhi maelfu wengine, kulingana na Balozi wa Iran, Amir Saeid Iravani.
Israel pia ilitekeleza mashambulizi mapya dhidi ya Lebanon Jumamosi baada ya wanamgambo wa Kiislamu wanaoegemea Iran, Hezbollah, kufyatua risasi kote mpakani.
Israel ilionya Lebanon kuhusu “gharama ghali mno” ikiwa haitadhibiti wanamgambo wa Hezbollah, huku idadi ya vifo kutokana na mashambulizi ya Israel nchini Lebanon tangu Jumatatu ikipanda na kufikia 300.
Mar 08, 2026 at 12:25PM
SERIKALI imeagiza kila kaunti ndogo kuanzisha vituo vya taarifa kwa umma, vituo vya dharura na vituo vya kukabiliana haraka na mafuriko ili kuwasaidia wananchi wanaokumbwa na maafa.
Hii ni baada ya miundombinu muhimu kuharibiwa vibaya katika maeneo mbalimbali ya nchi kutokana na mito kufurika na maji kuharibu barabara na daraja.
Katika Makueni, Barabara ya Wote–Emali pamoja na daraja la Kyamelu zilifurika na kuathiri usafiri. Bungoma, daraja la watembea kwa miguu la Kimama lilisombwa na mafuriko.
Katika Migori, daraja kwenye mto Migori pia liliharibiwa vibaya baada ya kusombwa na maji ya mafuriko.
Jijini Nairobi, angalau shule 15 zimeathiriwa, huku madarasa na vifaa vya shule vikiharibiwa na maji ya mafuriko.
Rais William Ruto alisema mafuriko hayo yamesababisha mateso makubwa kwa familia nyingi nchini.
“Mafuriko yanayoendelea katika sehemu za Nairobi na maeneo mengine ya nchi yamesababisha vifo vya kusikitisha,” alisema Rais katika taarifa aliyochapisha kwenye mtandao wa X.
Mkuu wa Mawaziri, Musalia Mudavadi, alisema hali ya mafuriko katika Nairobi ni ya kutia wasiwasi na haikubaliki.
Mar 08, 2026 at 12:16PM
Anayetupambia ukurasa huu leo ni Bi Kelsey Waweru, mwanabiashara katika Kaunti ya Nairobi. Uraibu wake ni kuogelea, kuchora na kucheza tenisi. PICHA| JOHN NJOROGE
Mar 08, 2026 at 11:35AM
JUHUDI za kuzima vuguvugu la Linda Mwananchi zinaendelea kufichuka huku likiendelea kufanya mikutano ya kisiasa nchini.
Kiongozi wa kundi hilo na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna anadai kuwa kuna juhudi za makusudi za kuzima shughuli zao, kuanzia kuvurugwa kwa mikutano yao, madai ya kujaribiwa kununuliwa kwa fedha nyingi hadi kuzuiwa kwa mipango ya kidijitali ya kuratibu shughuli zao.
Akizungumza katika mkutano wa People’s Dialogue Festival uliofanyika Uhuru Park, Sifuna alisema kundi lake limekumbana na vikwazo mara kadhaa tangu lianze mikutano ya Linda Mwananchi kote nchini.
“Tunafahamu kuna propaganda eti tuliitisha hadi Sh2 bilioni ili tusitishe kampeni yetu. Lakini vuguvugu hili ni kubwa kuliko mtu mmoja, hatutakubali kununuliwa,” alisema Sifuna.
Mikutano yao ya kisiasa imekumbwa na vurugu au vizingiti vinavyodaiwa kulenga kupunguza ushawishi wao.
Seneta wa Siaya James Orengo, ambaye pia amehusishwa na msimamo mkali wa kuikosoa serikali ya sasa, amewahi kuonya kuhusu kile alichokiita juhudi za kuzuia maoni tofauti katika siasa za Kenya.
Orengo amesisitiza mara kadhaa kuwa demokrasia haiwezi kustawi ikiwa makundi ya kisiasa yatazuiwa kuwasilisha maoni yao hadharani. “Katika demokrasia, lazima kuwe na nafasi ya sauti tofauti kusikika bila vitisho au vikwazo,” amewahi kusema katika mikutano ya kisiasa na mahojiano ya vyombo vya habari.
Mbali na kuvurugwa kwa mikutano, viongozi wa Linda Mwananchi pia wanadai kuwa kuna juhudi za kuwapa baadhi yao pesa ili waachane na vuguvugu hilo.
Sifuna alisema propaganda pia zimesambazwa zikidai kuwa aliomba pesa ili aachane na kampeni dhidi ya serikali jumuishi.
“Walianza kueneza propaganda kwamba nimeomba pesa ili kuacha vuguvugu hili. Ukweli ni kwamba sisi hatutayumbishwa na fedha,” alisema.
Kundi hilo pia linadai kuwa juhudi zao za kuanzisha tovuti na nambari ya kuchangisha pesa kutoka kwa wafuasi zimekuwa zikitatizwa mara kadhaa.
Kwa mujibu wa Sifuna, wafuasi wao walitaka kutumia mifumo ya kidijitali kuratibu mikutano na michango ya kuendesha kampeni za Linda Mwananchi, lakini mipango hiyo imekuwa ikizuiwa.
“Tumekuwa tukijaribu kuanzisha tovuti na nambari ya kuchangisha fedha lakini kila mara tunakumbana na vikwazo,” alisema.
Katika hatua nyingine iliyoibua utata, viongozi wa kundi hilo wanapinga jaribio la kusajili chama kipya kiitwacho "Linda Mwananchi Party.”
Kupitia mawakili wao, Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino waliwasilisha malalamishi kwa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa wakisema hawahusiki na juhudi hizo.
Walionya kuwa kusajili chama hicho kunaweza kuwapotosha wafuasi na hata kutumiwa vibaya kukusanya fedha kwa jina la vuguvugu lao.
Kulingana na mchanganuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki, mpango wa kusajili jina la vuguguvu hilo kama chama ni mkakati wa kulizima.
Anasema hatua ya ODM kumvua Sifuna wadhifa wake wa Katibu Mkuu ni sehemu ya mkakati wa kuzima ushawishi wa Linda Mwananchi unaoendelea kuongezeka.
Ingawa uamuzi huo ulizuiwa na mahakama kwa muda, wafuasi wa Linda Mwananchi wanadai kuwa hatua hiyo ilikuwa sehemu ya mkakati mpana wa kudhoofisha vuguvugu lao ndani ya chama.
Mvutano huo unajiri wakati ODM inakabiliwa na mgawanyiko wa ndani kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027 huku makundi mawili makuu –Linda Mwananchi linalokosoa ushirikiano wa kisiasa na serikali, na Linda Ground linalounga mkono ushirikiano huo yakikosoana.
Chama hicho kinatarajiwa kufanya mkutano wa wajumbe baadaye mwezi huu ambao dalili zinaashiria utaendeleza mgawanyiko baada ya wafuasi wa Linda Mwananchi kupinga ajenda zilizowekwa.
Wadadisi wa siasa wanasema kuvurugwa kwa mikutano ya Linda Mwananchi na maafisa wa usalama huku ile ya Linda Ground inayoongozwa na kiongozi wa ODM Oburu Odinga ikifanyika kwa amani ni ishara ya mkakati mpana wa kuzima vuguvugu hilo.
Huku mvutano ukizidi, wachambuzi wa siasa wanasema mbinu zinazodaiwa kutumika kuzima Linda Mwananchi zinaendelea kujenga kundi hilo linaloungwa mkono na vijana ambao ndio wengi nchini.
“Ni wazi kuwa kila uchao kuna njama zinazosukwa kuzima Linda Mwananchi ikiwemo madai ya mbunge mmoja kuhusisha jina hilo na kauli au shughuli za kijeshi. Wasichojua wanaofanya hivyo ni kuwa wanaendelea kulijenga jina hilo. Vuguvugu linaloanzishwa na watu huwa na nguvu zinazoweza kushinda muungano wa tabaka la wanasiasa wenye ushawishi,” akasema mchambuzi wa siasa Diana Avisa.
Mar 08, 2026 at 10:48AM
KUTANGAZA kwa mbunge wa Wundanyi Danson Mwashako kuwa atawania kiti cha ugavana Kaunti ya Taita Taveta na kudinda kuunga mkono serikali kwa awamu ya pili kunaonekana kumtia taabani kisiasa.
Msimamo wake wa kisiasa unaonekana kuwapa wengi tumbojoto, ikiwemo serikali kuu kwani anajitetea kwa kudhihirisha kuwa yeye ni mchapa kazi jambo ambalo limekuwa tishio kwa wawaniaji wengine.
Wiki hii, serikali kuu ikiongozwa na Naibu Rais Kithure Kindiki walizuru Kaunti ya Taita-Taveta ajenda kuu ikiwa kushawishi mbunge huyo ambaye ameonekena kuongoza wakazi wa Wundanyi kwa mihula miwili.
Hili limefanyika siku chache tu baada ya muungano wa wabunge kutoka kaunti sita za Pwani (CPG) kumng’atua mamlakani Bw Mwashako kama mwenyekiti wa muungano huo na kumchagua mwakilishi wa wanawake wa Kilifi Getrude Mbeyu kwa nafasi yake.
Uchaguzi huo ulionekena kama njia moja ya kumwadhibu mbunge huyo wa Wundanyi kwa kutounga mkono Rais William Ruto kwa awamu yake ya pili ya urais mwaka wa 2027.
Bw Mwashako, ambaye ni mbunge aliyechaguliwa kwa tiketi ya Wiper Patriotic Party ambaye alionekana kukataa kujiunga na chama cha UDA huku gavana wa sasa Andrew Mwadime ambaye alichukua uongozi kama mgombea huru akiingia katika mtego wa serikali na kujiunga na chama hicho.
Bw Kindiki katika ziara yake naye ameapa kutumia njia zote kumshawishi Bw Mwashako kutoshirikiana na upinzani.
“Wapi Danson Mwashako? Amehepa? Lazima aingie kwa serikali. Akiendelea kufuatana na watu wa DCP, tutamsafirisha,” Naibu wa rais Kindiki alionya Bw Mwashako.
Hivi karibuni, Bw Mwashako ambaye ameshikilia msimamo wake wa kutojiunga na serikali, amekuwa mstari wa mbele kukashifu uongozi wa Rais William Ruto akiwa na kundi la Linda Wananchi linaloongozwa na Gavana wa Siaya James Orengo, Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na mbunge wa Embakasi kusini Babu Owino.
Katika mahojiano na wanahabari baada ya ziara ya Bw Kindiki Kaunti ya Taita-Taveta mapema wiki hii, Bw Mwashako alikashifu serikali kwa kuwahadaa wakazi kwa kuzindua miradi miezi michache kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027.
“Kama ni haki yetu kujengewa barababra ya Voi kwenda Sagalla mbona wanaijenga sasa na hawakuianza mwaka jana kama walijua kwamba watu wa eneo hili ni wa muhimu? Haimaanishi kwamba kama mimi siko katika chama tawala, tuwapokonye wakazi wa Taita-Taveta miradi ya barabara, na kama watafanya hivyo, hawastahili kuwa katika uongozi kwani hawastahili kushikilia maendeleo eti kwa sababu hatuko nao,” alisema Bw Mwashako.
Hata hivyo, wachanganuzi wanamuonya Bw Mwashako kutojiunga na chama cha UDA iwapo anataka azma yake kuwa gavana itimie kwani serikali imekuwa na njama nyingi na Bw Mwadime ambazo Bw Mwashako amekuwa akizipinga.
“Bw Mwashako akikubali kuingia UDA atapambana na Bw Mwadime kwa mchujo ambaye amekuwa kipenzi cha serikali na kama njia ya kumwadhibu, watamnyima cheti dakika ya mwisho wakati hawezi kuhamia chama kingine,” alisema Bw Elijah Mwarondo, mkazi wa Wundanyi.
Mbunge huyo wa Wundanyi ameonekana mmoja wa viongozi ambao wako na nafasi kubwa ya kuchukua uongozi wa Kaunti hiyo mwaka wa 2027 kutokana na sifa za miradi aliyotekeleza katika eneobunge la Wundanyi kwa mihula miwili iliyopita.
Bw Mwashako hata hivyo, anatarajiwa kupata upinzani mkali kutoka kwa Seneta wa sasa Jones Mwaruma, Bw Mwadime, aliyekuwa Gavana wa kwanza Bw John Mruttu na mwenzake Bw Granton Samboja, pamoja na aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Halmashauri ya Bandari nchini (KPA) John Mwangemi.
Hadi sasa, hakuna mwanamke ambaye ametangaza nia ya kuwania kiti cha ugavana katika Kaunti ya Taita Taveta, huku wagombea wote waliotangaza nia yao wakiwa ni wanaume.
Hata hivyo, kunasubiriwa iwapo wagombeaji hao watatii pendekezo la wazee kutoka Kaunti hiyo kuwapiga msasa kabla ya kuingia debeni.
Hivi majuzi, viongozi na wazee kutoka maeneo bunge ya Mwatate, Wundanyi, Voi na Taveta wamekuwa wakijadiliana jinsi ya kutoa viongozi mwaka ujao ambao watatimiza mahitaji yao.
Tangu kuanzishwa kwa ugatuzi, Kaunti ya Taita Taveta imekuwa na laana ya ‘Wantam’ kwani imeongozwa na magavana watatu: Mhandisi Mruttu (2013–2017), Bw Samboja (2017–2022), na Gavana wa sasa Bw Mwadime.
Kiongozi wa muungano wa wazee hao Bw Thomas Mwadeghu amesema ijapo kisheria na kikatiba kila mmoja ana haki ya kugombea kiti chochote cha siasa, muhula huu wa kisiasa utakuwa tofauti kwani wakazi wa eneo hilo wamehadaiwa kwa muda na viongozi waliotangulia.
“Viongozi kutoka miungano mbalimbali eneo la Taita na Taveta wanaungana kutoa mwelekeo wa kisiasa na licha ya wagombeaji kutokea wengi, tunatarajia kufanya mchujo kulingana na matakwa ya wakazi,” alisema Bw Mwadeghu.
Mar 08, 2026 at 09:24AM
GAVANA wa Siaya, James Orengo ameshinikiza kuachiliwa huru kwa baadhi ya wasaidizi wake na wafanyakazi wa serikali yake aliodai walikamatwa Jumamosi, Machi 7, 2026, siku moja kabla ya ziara ya Rais William Ruto katika kaunti hiyo.
Kupitia ujumbe kwenye akaunti yake ya mtandao wa X siku hiyo, Bw Orengo alidai kuwa watu hao walikamatwa Siaya na Nairobi saa za jioni na kuzuiliwa na polisi, akitaja kitendo hicho kama ukiukaji wa katiba na misingi ya kidemokrasia.
“Jioni hii (Machi 7, 2026) wafanyakazi kadhaa wa serikali yangu walikamatwa kiholela na polisi na kuzuiliwa Siaya na Nairobi kuhusiana na ziara ya rais Siaya Jumapili, Machi 8, 2026. Vitendo vibovu kama hivi vya polisi havina nafasi chini ya Katiba ya sasa inayoheshimu demokrasia. Nataka waachiliwe huru mara moja,” Bw Orengo akaeleza, bila kutaja majina ya watu hao aliodai walikamatwa na polisi.
Rais Ruto anazuru Siaya mnamo Jumapili kuhudhuria sherehe ya kutoa shukrani kufuatia kuteuliwa kwa Katiba wa Wizara anayesimamia Huduma za Matibabu Dkt Ouma Oluga, katika Shule ya Msingi ya Okela, Uyoma, eneo bunge la Rarieda.
Rais anazuru Siaya wakati ambapo migawanyiko na uhasama inashuhudiwa ndani ya chama cha ODM na kufuatia kuibuka kwa mirengo miwili ya “Linda Ground” na “Linda Mwananchi”.
Bw Orengo anaegemea mrengo wa Linda Mwananchi unaoongozwa na Katibu Mkuu anayepigwa vita Edwin Sifuna na unaopinga ushirikiano wa chama cha ODM na kile cha UDA chini ya serikali jumuishi.
Mrengo huo pia unapinga kuchaguliwa tena kwa Rais Ruto ukishikilia kuwa ODM itadhamini mgambea Uraia katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Nao mrengo wa Linda Ground unaoongozwa na kiongozi wa chama Oburu Oginga na mwenyekiti Gladys Wanga, unaunga mkono ushirikiano wa vyama hivyo viwili huku ukirindima “injili” ya kuchaguliwa tena kwa Dkt Ruto katika uchaguzi mkuu ujao.
Mar 08, 2026 at 08:55AM
MBUNGE mwakilishi wa jinsia ya kike Kaunti ya Kisumu Ruth Odinga amemtembelea kiongozi wa chama cha Orange Democratic Movement (ODM) Oburu Odinga huku kukiwa na madai ya migawanyiko ndani ya chama hicho.
Kupitia taarifa aliyochapisha kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii Alhamisi, Machi 5, 2026, Ruth ambaye pia ni Katibu wa Uratibu wa ODM, alisema mazungumzo yao yalilenga kuimarisha umoja na mshikamano ndani ya chama pamoja na mikakati ya kupeleka mbele ajenda za kitaifa.
“Leo alasiri nilifanya ziara ya heshima katika afisi ya kiongozi wa chama cha ODM, Oburu Odinga, nikiwa na Mheshimiwa Catherine Omanyo. Tulikuwa na mazungumzo ya maana kuhusu kuimarisha umoja na mshikamano ndani ya chama na kuendeleza malengo ya kitaifa yanayowahusu Wakenya wote,” alisema.
Ruth alikuwa ameandamana na Omanyo ambaye ni naibu katibu mkuu wa chama hicho. Omanyo alipandishwa cheo hivi majuzi baada ya kuondolewa kwa Edwin Sifuna, hatua ambayo baadaye ilibatilishwa na Jopo la Kutatua mizozo ya vyama vya kisiasa (PPDT).
Ziara hiyo ilijiri huku kukiwa na madai kwamba kuna mvutano kati ya Ruth na kaka yake, Oburu. Hata hivyo, alikanusha madai hayo akisema wito wake wa kutaka utaratibu ndani ya ODM haufai kuchukuliwa kama ugomvi kati yake na kaka yake.
Alisema hana sababu ya kupigana na kiongozi huyo wa chama, akieleza kuwa wito wake umekuwa kuhimiza makundi ya “Wantam” na “Tutam” ndani ya chama kushirikiana na kuzungumza kwa sauti moja.
Ruth pia alisisitiza kuwa sauti za vijana zinapaswa kujumuishwa katika maamuzi ya chama, akisema hilo halipaswi kuchukuliwa kama dharau kwa seneta huyo wa Siaya.
Alifafanua kuwa mara nyingi humshauri Oburu kuhusu masuala mbalimbali ya chama na kisiasa, akiongeza kuwa kutoa maoni yake ndani ya chama cha kidemokrasia kama ODM hakumaanishi kuwa anapinga uongozi wake.
“Oburu ndiye kiongozi wa chama cha ODM na kila mtu anapaswa kuheshimu hilo. Ninazungumza naye mara kwa mara kama kiongozi wa chama na pia kama kaka yangu mkubwa. Lakini baadhi ya watu wameeneza wazo kwamba ninapigana naye,” alisema.
Aliongeza kuwa wanaodai anagombana na Oburu ndio maadui wa kweli wa ODM kwani chama hicho kinaruhusu wanachama wake kutoa maoni yao kwa uhuru.