Tue
21
Apr
26
Apr 21, 2026 at 12:32PM
KITOTO, Makueni: KIOJA kilishuhudiwa katika harusi moja hapa keki ilipokataa kukatika hadi mwenye kuipika alipolipwa deni lake. Inasemekana kila kitu kilionekana kuenda sawa hadi wakati wa kukata keki ulipofika. Bw Harusi na Bi Harusi walisonga mbele ya wageni kuikata na kuinua kisu kwa bashasha. Hata hivyo, walipojaribu kukata keki, haikukubali kabisa! Walijaribu mara kadhaa bila mafanikio, huku wageni wakishangaa. Ilibainika kuwa mpishi hakuwa amelipwa alivyokuwa amekubaliana na maharusi na alitumia mazingaombwe yake. Baadaye alitumiwa pesa kwa simu huku emcee akifanyia mzaha tukio hilo kuficha ukweli kisha kesi ikakubali kukatika kwa urahisi sana.
Apr 21, 2026 at 07:55AM
WAKIUNGWA mkono na vijana wa Gen-Z wanaozidi kuwa wakakamavu kwa usemi, sura mpya za wanasiasa zinajitokeza kama wagombea muhimu katika kinyang’anyiro cha 2027. Kundi hilo jipya la viongozi tayari linashinikiza mabadiliko ya kizazi ndani ya vyama vyao kwa kushindana moja kwa moja na vigogo wakongwe au kuamua kuanzisha mkondo wao tofauti kisiasa kabla ya uchaguzi mkuu ujao. Kuinuka katika umaarufu kitaifa kumewaweka katika nafasi ya kuwania nyadhifa kuu za uchaguzi, ukiwemo urais. Huku tasnia ya kisiasa ikizidi kubadilika, vigogo wa tangu jadi kisiasa, wanakodolea macho kudidimia kisiasa nao wanasiasa wachanga wakiwakabili ana kwa ana. Katibu Mkuu wa ODM, Edwin Sifuna na Mbunge wa Kiharu Ndindi Nyoro ni miongoni mwa wanasiasa vijana waliojitokeza zaidi nchini. Wote wawili wametajwa miongoni mwa wagombea ambao huenda wakawania kiti cha urais 2027. Wengine ambao wamegeuka wanasiasa mashuhuri kuelekea chaguzi wanajumuisha Mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino, Seneta wa Nyandarua, John Methu, Mwakilishi Mwanamke Kirinyaga, Njeri Maina, Mbunge wa Nyali, Mohammed Ali, na naibu kinara wa DCP Cleophas Malala. Bw Sifuna ndiye kinara wa Linda Mwananchi, kundi linalokua kwa kasi lililojitenga kutoka ODM ambalo linapinga serikali ya muungano na uongozi wa Dkt Oburu Oginga. Bw Sifuna ametajwa kama anayeweza kuwa mgombea urais wa kundi hilo hatua itakayobadilisha mipangilio ya ODM na mwelekeo wa kinyang’anyiro cha 2027. Kambi hiyo inayoonekana kuwiana vyema na wapigakura vijana, imeshiriki misururu ya mikutano ya hadhara kote nchini ikijitahidi kuzindua mchango wa umma, kurejesha utawala wa kikatiba na kuunganisha uongozi wa kisiasa na uhalisia mashinani. Bw Nyoro, 40, kwa upande mwingine, amevutia umaarufu kama mbunge mwenye ufasaha na anayeoongozwa na sera. Japo angali mwanachama wa UDA, ameibuka kuwa moja kati ya wakosoaji sugu wa serikali ya Kenya Kwanza. “Viongozi kama vile Sifuna, Nyoro na Babu wanaashiria kuinuka kwa kizazi cha wahusika stadi kisiasa,” anasema mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Moi, Profesa Masibo Lumala. Anasema Sifuna, hasa, anajitokeza kwa njia ya kipekee sio tu kwa azma, bali weledi kisiasa kimaksudi huku akijiweka kwenye nafasi ya kugombea urais 2027. “Nguvu za Nyoro zipo kwenye uadilifu wa tabaka tawala na msingi wa kisera, huku Babu Owino akijivunia ngome imara inayoegemea uanaharakati unaounda simulizi za siasa za maeneo ya mijini.” “Kwa pamoja, wataathiri ajenda na uhamasishaji 2027. Hata hivyo, ugombea urais wa Sifuna unapima kwa njia ya kipekee iwapo uwaniaji unaoendeshwa na ujumbe na vijana unaweza kubadilisha mwonekano na uwiano kuwa uwezo wa kuchaguliwa kitaifa katika mpangilio wa kisiasa nchini,” anafafanua Profesa Masibo.
Apr 21, 2026 at 06:55AM
KWA muda wa miaka 10, Duncan Kibet, mchuuzi wa bidhaa katika Kaunti ya Bomet amekuwa akijaribu kujiunga na chuo kikuu, apate shahada ili kuimarisha hali ya maisha ya familia yake changa. Licha ya juhudi hizo, Bw Kibet, 27 amekuwa akihangaika kwa kukosa karo. Alisomea Shule ya Msingi ya Kipkoligo kabla ya kujiunga na Shule ya Tenwek Boys, Kaunti ya Bomet ambako alipata alama ya C+ kwenye Mtihani wa Kitaifa wa Kidato cha Nne (KCSE) mnamo 2015. Licha ya kupata alama hiyo, hakuweza kujiunga na elimu ya chuo kikuu kutokana na changamoto za kifedha. Hivi majuzi baba huyo wa mtoto mmoja alitembea kilomita 250 kutoka kijiji cha Kipkoligo, Chamaner Kaunti ya Bomet hadi Nairobi akilenga kupata karo. Hata hivyo, anasema juhudi hizo hazikumletea fedha. “Mnamo Januari 28, 2026 nilitembea hadi Nairobi kupata karo baada ya kukaa nyumbani kwa miaka 10 wakati ambapo nilifanya kazi za mikono. Ilinichukua siku nne kufika Nairobi ambako marafiki walikuwa wenyeji wangu,” akasema. Wakati wa safari hiyo alilala kwenye nyumba ya jamaa zake Narok, Ntulele, Mai Mahiu na baadaye kwenye nyumba za msamaria Nairobi. Kwa wiki tatu akiwa Nairobi, Bw Kibet aliwaomba wahisani wamsaidie kabla ya kurejea Bomet bila pesa za maana za kufadhili masomo yake. “Bado sijafua dafu katika kupata karo na nawaomba wahisani waje wanisaidie,” akasema. Kisa chake hivi majuzi kilivutia umma na akasajiliwa kujiunga na Chuo Kikuu cha Mlima Kenya kusomea fasihi ya Kingereza. Mbunge wake Richard Yegon (Bomet Mashariki) alimlipia Sh71,000 kugharimia masomo ya muhula mmoja pamoja na Sh6,000 za malazi. Bw Kibet anatarajiwa kujiunga na chuo hicho mnamo Aprili 27 huku makataa ya kujisajili yakiwa ni Aprili 30. Viongozi kadhaa wameahidi kuwa watamsaidia kufadhili masomo yake lakini wengi bado hawajatuma hela. Kwa sasa Bw Kibet ana wingu la matumaini kuwa atapata hela za kutosha kusaidia kufadhili elimu yake.
Apr 21, 2026 at 05:55AM
JE, umewahi kufahamu kuwa maganda ya matunda yanaweza kutumiwa kutengeneza malighafi muhimu katika hatua ya ukuaji wa viwanda? Hii ndiyo hali halisi katika Shule ya Msingi ya Wasichana ya St Marys inayopatikana Kaunti ya Nakuru. Wanafunzi wa kundi la Sayansi hutengeneza mafuta aina ya ethanol kutokana na maganda ya mananasi. Uvumbuzi ambao wanaamini si tu wa manufaa kwao bali kwa kizazi kijacho hususan miongoni mwa wanafunzi ambao wanalenga kuzamia kozi ya uhandisi siku zijazo. Hapa tunakumbana na mwanafunzi Joy Waruguru mwenye umri wa miaka 14 na pia kinara wa wanafunzi klabu ya Sayansi. Anasema alipata wazo la kutengeneza malighafi hii muhimu kutokana na maganda ya matunda baada ya kubaini kuwa msambao wa taka ni kero kwa wakazi wengi wa mijini. Aidha, sehemu nyingi za kuuzia vyakula humu nchini hususan sokoni hazina mpangilio madhubuti wa kutupa taka hizi. Hatua ambayo hatimaye husababisha mrundiko wa takataka na pia kusababisha maradhi ya kuambukizana. Waruguru anasema kwa ushirikiano mkubwa baina yake, wanafunzi wenzake na pia mwalimu kinara wamegundua kuwa maganda ya mananasi yanaweza kutengeneza mafuta aina ya Ethanol. Anafafanua kuwa kabla ya kuwasilisha teknolojia hii kwenye maonyesho ya Kisayansi ya kila mwaka kwa shule za Msingi nchini, walipata fursa ya kuwasilisha kwa wanafunzi wenzao. "Walituhimiza na kututia moyo kutokana na uvumbuzi huu wa kipekee ambao unazingatia kiwango cha juu cha ubunifu," asema. Aidha, walipokuwa wakiendelea na mchakato wa kujiandaa kabla ya mashindano waliunda utaratibu wa kusawazisha muda wao wa darasani na ule wa shughuli hii. Isitoshe, anawahimiza wanafunzi kujiunga na vyama vya Sayansi shuleni mwao ili kutoa suluhu ya kudumu kwa changamoto nyingi zinazolemaza maendeleo nchini. Anasema hii itakuwa hatua muhimu sana hasa katika sekta ambazo zimekuwa zikikumbana na changamoto tele kila kukicha.
Apr 21, 2026 at 04:55AM
BWANYENYE wa Mombasa, Abu Joho, ambaye pia ni ndugu wa Waziri wa Madini na Uchumi wa Bahari, Hassan Joho, amewahimiza vijana wa Pwani kutokata tamaa maishani na badala yake wajitume katika masomo na kutafuta fursa bora za maisha. Akizungumza katika eneo la Changamwe, Bw Abu aliwataka vijana kuzingatia elimu hadi vyuo vikuu na vya kiufundi badala ya kukaa kwenye maskani bila mwelekeo. Alitoa mfano wa nduguye Bw Joho, ambaye alisema alipata alama ya D- lakini baadaye aliendelea na masomo hadi kufika chuo kikuu na kufanikiwa hata kuwa Gavana wa kwanza wa kaunti ya Mombasa, na sasa ni Waziri katika serikali ya Kenya Kwanza. “Nani ana B na hajaenda chuo kikuu? Msikate tamaa. Angalieni Hassan Joho alipata D- lakini aliendelea hadi chuo kikuu hata kile cha Harvard. Mungu, nidhamu na bidii ndio msingi wa mafanikio,” alisema. Bw Abu alisema ataendelea kuzuru maskani mbalimbali katika kaunti ya Mombasa ili kuwatafuta vijana wasio na uwezo na kuwasaidia kupata ajira au kujiunga na vyuo vikuu. “Ninawaahidi kuwa nitakuwa nikizuru maskani kuchagua vijana mwenyewe ili niwasaidie kupata ajira au wale wanaotaka kuendelea na masomo niwalipie karo. Nataka kusaidia yule asiye na mbele wala nyuma, yule ambaye amekata tamaa na hana wa kumtegemea isipokuwa Mungu,” alisema. Aliongeza kuwa tayari ameajiri vijana wengi kutoka maskani na ataendeleza mpango huo. Katika eneo la Changamwe, alisema alichukua stakabadhi za vijana wenye shahada na kuahidi kuwasaidia kupata ajira. Mwaka jana alisaidia zaidi ya vijana 10 kutoka mtaa wa Maweni kujiunga na vikosi vya polisi kupitia juhudi zake. Hata hivyo, aliwaonya vijana dhidi ya kutumiwa na wanasiasa kuzua vurugu katika mikutano kwa ajili ya fedha. Kwa wale ambao hawakufika kidato cha nne, Bw Joho alisema atawasaidia kupata vibarua ili waweze kujitegemea. Alibainisha kuwa ameunda kikundi maalum cha kusaidia vijana wa Mombasa kupata ajira au kujiendeleza masomo. Alisema kupitia juhudi hiyo ameweza kufanikiwa kuwabadilisha baadhi ya vijana waliokuwa wakijihusisha na uhalifu. “Kuna waliokuwa wakibeba mapanga lakini sasa wameacha uhalifu na wanafanya kazi halali kwa sababu tuliwasaidia,” alisema. Vile vile, aliwasihi vijana kujiandikisha kuwa wapigakura ili kushiriki kikamilifu katika kuchagua viongozi.
Apr 21, 2026 at 03:55AM
KIONGOZI wa ODM, Dkt Oburu Oginga ametangaza kuwa mara hii chama hicho kitaandaa uteuzi wa haki na huru wala hakuna atakayependelewa kutokana na ukuruba wake na uongozi wa chama. Dkt Oginga aliwaambia vijana wajitokeze kuwania viti kupitia ODM, akisema chama hicho kina mikakati ya kuanza kuchangamkia viongozi vijana mwaka wa 2027. “Chini ya uongozi wangu nitahakikisha kuwa uteuzi ni huru na haki na vijana watakuwa na nafasi yao,” akasema Dkt Oginga, 82. Alikuwa akiongea jana wakati wa Kongamano la Vijana wa ODM katika uwanja wa Jamuhuri Nairobi. Hafla hiyo ilihudhuriwa na vigogo wa ODM akiwemo Mwenyekiti Gladys Wanga na Waziri wa Madini Hassan Joho. Kauli ya Dkt Oginga inakuja huku chama hicho kikipoteza viti kwa wapinzani miaka ya nyuma kutokana na mapendeleo kwenye uteuzi au kutoa tikiti za moja kwa moja. Kwenye uchaguzi mkuu wa 2022, chama hicho kiliachia Jubilee kiti cha ugavana Nairobi licha ya kuwa mgombeaji wao Tim Wanyonyi (Mbunge wa Westlands) alikuwa na umaarufu na ugavana ukaishia kunyakuliwa na UDA. Jana, Dkt Oginga aliweka bayana kuwa hawataingia mkataba wowote wa kuachiana viti Nairobi, akisema kuwa ODM inalenga kudumisha na hata kuongeza idadi ya viti vya ubunge. “Tunalenga viti vingi zaidi ila lazima tuhakikishe watu wetu wanajisajili ndipo tuwe na kura nyingi,” akasema mbunge huyo wa Bondo. ODM imekuwa ikikabiliwa na maasi ya ndani ambapo kumeibuka makundi ya Linda Mwananchi na Linda Ground anayoingoza Dkt Oginga. Jana alionekana akimlenga Katibu Mkuu Edwin Sifuna, akidai kuwa hawezi kuruhusu chama kugawanywa na viongozi wanaoenda kinyume na kinachokubaliwa kwenye mikutano ya viongozi wa ODM kisha kudai ni haki yao. “Chama hakiwezi kuwa na fujo kupitia viongozi wanaosema mambo yao ya kibinafsi hapo nje kisha kudai ni ya chama. Mtu mmoja hawezi kuchukua msimamo na kuzungumza jambo tofauti kisha adai ni msimamo wa chama,” akaongeza. Kauli yake iliungwa mkono na Gavana Wanga ambaye alisema ODM bado ni chama imara hata baada ya mauti ya Kinara wake Raila Odinga. Mwenyekiti wa chama Kaunti ya Nairobi George Aladwa alisema mifumo ya chama lazima ifuatwe kuhakikisha kuwa wanadumisha umaarufu wao Nairobi. “Tutamtetea kiongozi wetu wa chama na mnamo 2027 viti vyote vya ubunge Nairobi lazima ODM ivishinde. Binafsi nitakuwa nawania ugavana,” akasema Bw Aladwa. Kila kiongozi aliyehutubu kwenye hafla hiyo alisema kuwa ODM lazima iwe makini kwenye muungano wake na UDA ili chama kisimezwe.
Apr 21, 2026 at 02:55AM
RAIS William Ruto sasa amekumbatia mbinu mpya ya kusaka uungwaji mkono katika eneo la Mlima Kenya akisema kuwa ‘atarudisha mkono’ mwaka wa 2032 kwa kuunga naibu wake Prof Kithure Kindiki. Haya yanatokea baada ya Rais kupoteza ufuasi katika eneo hilo ambako alijizolea asilimia 87 ya kura mnamo 2022. Kiini cha masaibu yake ni kutimuliwa kwa aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua mnamo Oktoba 2024. Baada ya kutimuliwa, Bw Gachagua ameendelea kuwa mwiba kwa Rais Ruto baada ya kuanzisha chama cha DCP na kuongoza maasi dhidi ya Kiongozi wa Nchi eneo la Mlima Kenya. Bw Gachagua, baada ya kutimuliwa, amejenga himaya yake ya kisiasa eneo hilo na kumchora Rais Ruto kama adui wa jamii ya Mlimani. Juhudi ambazo Rais amekuwa akifanya kudumisha umaarufu wake eneo hilo hazijaonekana kuzaa matunda huku wandani wake wakizidi kuibuka na mikakati zaidi ya kuokoa hali. Ni changamoto hizi ambazo sasa zimemfanya Naibu wa Rais aanze kusawiriwa kama mrithi wa Rais Ruto katika uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2032. Rais, Prof Kindiki na baadhi ya wandani wao wamekuwa wakiashiria kuwa Prof Kindiki anaandaliwa kuwahi urais 2032. Akiwa katika ziara ya Kaunti ya Kisii, Rais Ruto alisema Bw Gachagua hana subira, jambo lililomchongea. “Ikiwa huna subira ya kuongozwa, hufai kuongoza,” akasema, kauli ambayo, ikitathminiwa sambamba na sifa ambazo amekuwa akimiminia Prof Kindiki, inaweka bayana siasa za urithi wa 2032. Jumatatu, Mbunge wa Kapseret, Oscar Sudi, mwandani wa Rais, alisema njia pekee ya Mlima Kenya kurejea Ikulu ni kupitia ushirikiano wa kisiasa kati ya Rais Ruto na Prof Kindiki. “Rais hafichi kuwa yeye ni zao la Mlima Kenya na angependa kushirikiana na eneo hilo sasa na siku zijazo katika kuunganisha nchi. Manaibu wanaoonyesha subira, uaminifu na bidii hufanikiwa, na Prof Kindiki ni mmoja wao,” akasema Bw Sudi. Kwa upande wake, Prof Kindiki amedokeza wazi kuwa uaminifu wake kwa Rais Ruto ni mkakati wa kisiasa ikizingatiwa kuwa yuko karibu na kiti cha urais. “Wakati mwingine si suala la mapenzi au kushabikia kiongozi ila ni kile ambacho unakilenga." “Rais Ruto ni kama ng’ombe wa maziwa mwenye mimba anayekaribia kuzaa na mimba hiyo ni mimi,” akasema Prof Kindiki. “Nikisalia karibu na Rais, kupanda kwangu kisiasa kutachukua miaka mitano. Ikiwa mtu mwingine atachukua nafasi hiyo 2027, tutasubiri muda mrefu zaidi,” akaongeza. Wandani wa Bw Gachagua, hata hivyo wamekosoa kauli hiyo wakisema Prof Kindiki analenga kutumia siasa za urithi kuvuruga miungano mipya ya kisiasa nje ya kambi ya Rais. Kwa mujibu wa mchanganuzi wa masuala ya kisiasa, Dkt John Okumu, mvutano kati ya Prof Kindiki na Bw Gachagua unaanika wazi jinsi ambavyo siasa za urithi za 2032 zimeanza kushika kasi hata kabla ya kura ya 2027. “Ni wazi kuwa Prof Kindiki na Bw Gachagua wanatofautiana kutokana na hesabu za uchaguzi wa 2027." “Faida ya mmoja ni hasara kwa mwingine ndiyo maana kuna mvutano mkubwa kati yao,” akasema Dkt Okumu. Dkt Okumu anaona nafasi ya Prof Kindiki ikifanana na mikakati ya awali ya urithi wa uongozi, akirejelea makubaliano ya mnamo 2013 kati ya aliyekuwa Rais Uhuru Kenyatta na mgombeamwenza wake wakati huo, William Ruto (sasa rais). Mchanganuzi mwingine Dkt Malila Munywoki naye anasema ni vigumu kwa Rais Ruto kutangaza wazi mpango wa urithi unaomhusisha Prof Kindiki kwa sasa. “Itakuwa vigumu kwa Rais kusema wazi ‘kumi yangu, kumi ya Kindiki’ kwani hilo linaweza kutenga maeneo mengine na miungano ya kisiasa,” akasema Bw Munywoki.
Apr 20, 2026 at 05:11PM
MAHAKAMA Kuu Jumatatu, Aprili 20, 2026 ilikataa ombi la wakili jijini Nairobi, Kimani Wachira, la kuitaka itoe amri ya dharura ili asikamatwe kwa tuhuma za kupokea Sh1 milioni ili kumhonga jaji. Jaji Roseline Aburili alisema Wachira hakutoa hoja nzito kwa nini ombi lake lishughulikiwe kama la dharura. Bi Aburili alisema wakili huyo tayari alikuwa ameachiliwa kwa dhamana ya Sh200,000 na Tume ya Maadili ya Kupambana na Ufisadi (EACC) na hakukuwa na ushahidi kuwa kuna kesi nyingine ya uhalifu dhidi yake. Badala ya kuridhia ombi lake, Mahakama ilimwaamrisha Wachira awasilishe nakala ya kesi kwa EACC, Mwanasheria Mkuu, aliyekuwa Waziri Raphael Tuju na Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma. Wachira alielekea kortini mnamo Machi akishutumu mashirika ya serikali akidai yalikuwa yakipanga kuwasilisha mashtaka ya utoaji hongo dhidi yake.

To continue using the website, you must be logged in.

Your login information is stored on your browser only.

OR

Support Our Website

Ads help us keep our content on kenyalivetv.co.ke free for you. Please consider supporting us by disabling your ad blocker or whitelisting our site in your ad blocker settings.

You are currently offline.
You are back online.