Sun
31
May
26
May 31, 2026 at 03:02PM
JASHO, presha na shamrashamra zilitawala katika toleo la tatu la mashindano ya Ndondi ya Rising Stars yaliyoandaliwa katika viwanja vya ASK Showground, Jamhuri jijini Nairobi Ijumaa. Mashindano hayo ya mapambano nane yaliyodhaminiwa na kampuni ya SportPesa na kuandaliwa na Maurice Odera kupitia Ultra Fight Series Boxing (UFS BXNG), yaliwashuhudia mabondia wakionyesha uwezo mkubwa huku Technical Knockouts (TKO) zikitoa burudani ya kiwango cha juu kwa mashabiki waliofurika ukumbini. TKO inamaana, kumalizika kwa mapambano kwa uamuzi wa kiusalama au wakati bondia anatupa taulo ndani ya ukumbi au kuomba pambano lisimamishwe. Pambano kuu kati ya Amos Amenya na Abdul Hakim lilikuwa kali kuanzia mwanzo hadi mwisho huku mabondia hao wawili wakibadilishana makonde na mbinu za kila aina kutafuta ushindi. Mapambano hayo yaliendelea hadi raundi ya sita kabla ya Amenya kumpiga Hakim kwa TKO na kutwaa ushindi katika pambano la uzani wa Super-Featherweight. Meneja wa Ushirikiano na Udhamini wa SportPesa, Japheth Akhulia, alisema moja ya vitu vinavyofanya mashindano hayo kuwa ya kipekee ni uwiano wa uwezo kati ya mabondia wanaoshiriki. “Kitu cha kipekee kuhusu SportPesa Boxing Rising Stars ni uwiano wa nguvu kati ya mabondia. Wale wanaokutana ulingoni huwa na nafasi sawa ya kuonyesha vipaji vyao,” alisema Akhulia. Aliwahimiza mashabiki kujitokeza kwa wingi kushuhudia mapambano hayo akisema, baadhi ya mabondia wanaoshiriki wana nafasi kubwa ya kuwa mastaa wa baadaye katika mchezo wa ndondi. Kauli yake iliungwa mkono na Mkuu wa Udhamini wa Kimataifa wa SportPesa, Alan McTavish, aliyesema walipanga kalenda ya mwaka 2026 kuhakikisha kuna mchanganyiko wa mashindano ya chipukizi pamoja na mashindano mengine. Wakati huo huo, bondia Jin Shen mwenye umri wa miaka 21 aliendelea kung’ara baada ya kumwangusha Elias Njoroge kupitia TKO katika raundi ya pili ya pambano lao la Bantamweight. Shen alipata ushindi wake wa pili mfululizo katika mashindano hayo baada ya kufanya vizuri pia kwenye mchezo wake ya kwanza Februari mwaka huu alipomshinda Jeremiah Abuko. “Niliweza kumshinda Njoroge kutokana na mazoezi mazuri ya nguvu na maandalizi makali niliyofanya,” alisema Shen. Aliongeza kuwa analenga kuendelea na kiwango hicho huku akiimarisha jina lake katika mchezo wa ndondi.  Matokeo ya Mapambano Welterweight (Raundi 4) Edwin Hayo alimshinda Moses Siviya Alama: 39-37, 38-38, 39-37 2.Super Lightweight (Raundi 4) McGregor Njoroge alimshinda Davis Gwaro Kwa TKO ((Raundi ya 3) 3.Featherweight (Raundi ya 4) John Logova alimshinda Muiruri Irungu Kwa TKO (raundi ya 1) Light Heavyweight (Raundi ya 4) Gentry Ochieng alimshinda Peter Wanda Kwa TKO ((Raundi ya 2) Lightweight (Rounds 4) Victor Oduor Andere alimshinda Dennis Ashley Alama: 40-36, 39-36, 40-36 Bantamweight (Raundi ya 4) Jin Shen alimshinda Elias Njoroge Kwa TKO (raundi 2) 7.Light Heavyweight (Raundi 4) Elijah Kingi alimshinda James Otieno Kwa TKO (raundi ya 1) Super Featherweight (Raundi ya 6) Amos Amenya alimshinda Abdul Hakim Kwa TKO (raundi ya 6)
May 31, 2026 at 10:55AM
MAMLAKA nchini Italia zimepiga marufuku tamasha mbili zilizopangwa kufanyika Julai katika mji wa Reggio Emilia na wanamuziki wa rapa wa Amerika, Kanye West na Travis Scott. Uamuzi huo ulitangazwa Jumamosi na mkuu wa serikali katika eneo hilo, Salvatore Angieri, ambaye alisema tamasha hizo zimefutwa kutokana na wasiwasi kuhusu usalama pamoja na uwezekano wa maandamano. Scott alifaa kutumbuiza katika Tamasha la Pulse of Gaia Julai 17 katika ukumbi wa RCF Arena huku Kanye West, anayejulikana pia kama Ye, akitarajiwa kutumbuiza watu siku iliyofuata. Kanye amekuwa akiandamwa na kufutwa kwa matamasha kadhaa barani Ulaya katika miezi ya hivi karibuni kufuatia matamshi yake ya kupinga Wayahudi. Mwanamuziki huyo amewahi kutoa kauli za kumsifu dikteta wa Ujerumani wa zamani, Adolf Hitler, na kuchapisha maudhui yaliyohusishwa na alama za msimamo wake dhidi ya Wayahudi. Matamshi hayo yalikosolewa na mashirika ya kutetea haki za binadamu na jumuiya za Wayahudi duniani. Kwa upande wake, Travis Scott ameendelea kukumbwa na maswali kuhusu usalama katika matamasha yake tangu tukio la mwaka 2021 katika tamasha la Astroworld mjini Houston, Texas, ambapo watu 10 walifariki na mamia kujeruhiwa baada ya umati mkubwa kusongamana. Angieri alisema uamuzi wa kufuta matamasha hayo ulifikiwa baada ya maombi kutoka kwa kundi moja pamoja na jumuiya ya Wayahudi katika mikoa ya Modena na Reggio Emilia, ambao walieleza wasiwasi wao hasa kuhusu ushiriki wa Kanye. Mamlaka pia zilisema kuwa muda mfupi kati ya tamasha hizo mbili na idadi kubwa ya mashabiki waliotarajiwa kuwasili ndani ya saa 24 uliongeza hatari za kiusalama. Aidha, walitaja kufutwa kwa matamasha mengine ya Kanye katika mataifa mbalimbali ya Ulaya kama "hatari halisi" ya maandamano makubwa dhidi ya mwanamuziki huyo. Hatua hiyo ni pigo jingine kwa Kanye, ambaye amekuwa akipoteza nafasi za kutumbuiza katika mataifa kadhaa kutokana na kauli zake zenye utata, huku mijadala ikiendelea kuhusu mipaka ya uhuru wa kujieleza na wajibu wa wasanii maarufu kwa jamii.
May 31, 2026 at 09:55AM
HUZUNI na majonzi zilitanda katika mochari ya Hospitali ya Kaunti Ndogo ya Naivasha jana huku familia, jamaa na marafiki wa wasichana 16 waliofariki katika mkasa wa moto katika Shule ya Upili ya Utumishi Girls wakianza shughuli ngumu ya kutambua miili ya wapendwa wao. Moto huo uliteketeza bweni la Meline Waithera Block B usiku wa Jumatano. Bweni hilo lilikuwa na wanafunzi 220 wa Gredi ya 10, Kidato cha Tatu na Kidato cha Nne. Wazazi wa wasichana hao 16, wakifuatana na jamaa zao, walifika hospitalini kwa shughuli ya uchunguzi wa maiti huku wakifarijiana katika kipindi hiki kigumu ambacho kimeacha nchi katika maombolezo. Madaktari watatu wa uchunguzi wa maiti wametumwa kuhakikisha zoezi hilo linakamilika haraka na kwa ufanisi. Uchunguzi huo unatarajiwa kusaidia kubaini chanzo halisi cha vifo hivyo pamoja na kurahisisha kutambua miili. Familia hizo pia zinasubiri matokeo ya vipimo vya DNA kabla ya kukabidhiwa miili kwa mazishi. Nje ya hifadhi ya maiti, jamaa walionekana wakiwa wamelemewa na huzuni. Wengine walikuwa wakisali huku wengine wakikumbuka maisha ya wasichana hao ambao ndoto zao zilikatizwa ghafla na moto huo. Wasichana wengine saba waliopata majeraha bado wamelazwa katika hospitali moja jijini Nairobi. Maafisa wa hospitali waliimarisha usalama katika eneo la mochari ili kudumisha utulivu wakati wa zoezi hilo muhimu. Ni wanafamilia wa karibu na wahudumu walioidhinishwa pekee kuingia. Shirika la Msalaba Mwekundu Kenya pia limeweka mahema katika eneo hilo, ambapo washauri nasaha na wanasaikolojia wanatoa huduma kwa familia zilizoathirika. Magari mawili ya ambulensi yamewekwa tayari kushughulikia dharura zozote za kiafya. Baada ya kuona miili hiyo, mmoja wa jamaa, Bw Njuki Nthimba, alisema ni miili mitatu pekee iliyoweza kutambuliwa kwa urahisi huku mingine ikiwa imeungua vibaya kiasi cha kutotambulika.
May 31, 2026 at 08:55AM
BAADHI ya wafuasi wake humuita Nyawawa (roho ya waliokufa), wengine humuita Nyatieng (jiwe linaloweza kuua) na kwa wengine yeye ni Wuod Nyamayanga (mwana wa kiume wa Nyamayanga). Licha ya majina hayo yenye sifa za ushujaa, Gavana wa Siaya James Orengo anakabiliwa na wakati mgumu katika taaluma yake ya kisiasa. Orengo, 75, ni kati ya wanasiasa ambao wamehudumu kwa kipindi kirefu zaidi katika nafasi za uongozi kutoka eneo la Nyanza. Aliingia bungeni 1979 akiwa na umri wa miaka 28. Hii leo jamii ya Waluo itakapokutana uwanjani Kirembe eneobunge la Kisumu Mashariki ili kutangaza mwelekeo wake wa kisiasa 2027, Orengo hatakuwepo. Gavana huyo kwa sasa yupo katika mvutano wa ubabe wa kisiasa na kinara wa ODM, Dkt Oburu Oginga. Aidha, Orengo amekemewa kutokana na matamshi ya kumdhalilisha Gavana wa Homa Gladys Wanga aliyoyatoa majuzi. Pia kuna uhasama kati yake na Naibu Gavana William Oduol pamoja na Bunge la Kaunti ya Siaya. Vile vile, anapambania ubabe kwenye mrengo wa Linda Mwananchi na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna. Hivi majuzi tu Orengo alilalamika kuwa maafisa wa ulinzi walikuwa wameondolewa kwenye makazi yake Nairobi, akihusisha tukio hilo na msimamo wake wa kisiasa. Mnamo Ijumaa mikutano yake ya kusaka uungwaji mkono Mbita, Kaunti ya Homa Bay, iligubikwa na ghasia huku magari yake yakishambuliwa na mlinzi wake kujeruhiwa vibaya. Katika Kaunti ya Siaya, Gavana Orengo hapumui kwa sababu mchakato wa kumtimua upo njiani. Kwenye mahojiano na Taifa Dijitali, Diwani Washington Booker ‘Dasani’ wa Uyoma Kaskazini alifichua kuwa anapanga kuwasilisha hoja ya kumtimua gavana huyo. “Nina hoja tosha ya kumtimua gavana, moja ikiwa kukosa kutekeleza miradi ilhali tuna bajeti kwa mwaka mzima wa fedha. Pia alitimua vibarua waliokuwa wamefanya kazi kwa mwaka mzima ilhali anasema hawajui,” akaeleza Booker. “Hazina ya fedha ya Siaya sasa inasimamiwa na mtu ambaye alikataliwa na Bunge la Kaunti. Nasaka saini 30, na jinsi mambo yalivyo hatima ya Bwana Orengo itakuwa mikononi mwa Bunge la Kaunti,” akaongeza. Hivi majuzi Orengo alijipata pabaya na shinikizo zinaendelea kumwandama kutokana na matamshi aliyoyatoa dhidi ya gavana mwenzake Wanga wakati akihutubia umma katika kituo cha mabasi mjini Homa Bay. “Orengo…wanawake kwenye siasa na uongozi wametoka mbali wala hatutarudi nyuma. Matusi na maneno ya kudhalilisha Gavana Wanga hayana nafasi katika siasa zetu,” akasema Mbunge wa Kisumu Mjini Magharibi, Rosa Buyu. Bado kwenye kaunti Orengo hapatani na naibu wake Oduol wawili hao wakikosana miezi michache tu baada ya kuingia mamlakani 2022, na sasa uhasama wao unatokota. Marehemu kinara wa ODM, Raila Odinga, ndiye aliwapatanisha kuelekea mchujo wa chama 2022 na wakawania kwa tikiti moja. Mnamo Mei 29, 2023, uhasama wao ulifikia kilele wakati Oduol alitimuliwa na madiwani ila akanusuriwa na Seneti mnamo Juni 26, 2023. Tangu wakati huo Oduol, ambaye anamezea mate ugavana, haonani uso kwa macho na bosi wake Orengo. Naibu gavana huyo pia amekuwa akitengwa kwenye shughuli za usimamizi wa kaunti. Oduol kwa sasa yuko mrengo wa Linda Ground ambao haupatani na ule wa Linda Mwananchi unaoshabikiwa na Orengo. Licha ya kutangaza kuwa atakuwa akiwania urais 2027 Gavana Orengo hajapata uungwaji mkono kutoka hata kwa mbunge mmoja wa eneo la Luo Nyanza. “Amejitenga na usimamizi wa kaunti na sasa anataka kuvuruga jamii ya Waluo. Anataka watu warejelee maandamano baada ya kifo cha Raila, lakini hatutakubali hilo,” akasema Mbunge wa Alego Usonga Samuel Atandi ‘Meli’. Hata hivyo, Orengo mwenyewe anasisitiza kuwa hatatishwa, na kwamba mkondo wa kisiasa ambao amechukua ndio utafaa Waluo. “Siasa zangu kila mtu anajua, na mara kwa mara nimekuwa upande wa wananchi. Wafanye kile wanataka lakini sitatetereka,” akasema Orengo. Kwa mujibu wa mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Profesa Lumala Masibo, gavana huyo wa Siaya anataka kuwa kigogo wa kisiasa za Luo Nyanza baada ya mauti ya Raila. “Hata huo urais hamakinikii, lengo lake anataka kuchukua chama kutoka kwa Oburu ili awe kigogo wa siasa wa Luo Nyanza. Kumbuka alijaribu kufanya hivyo Raila alipokuwa hai lakini hakufaulu,” aeleza Prof Masibo.
May 31, 2026 at 07:55AM
VUGUVUGU la Linda Mwananchi limeanza kuwika tena huku Linda Ground ikionekana kufifia, taswira inayodhihirisha mabadiliko mapya ya kisiasa yanayozidi kuchipuka kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027. Leo vuguvugu hilo linaloongozwa na Katibu Mkuu wa ODM na Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna, litafanya mkutano mkubwa Machakos katika kile kinachoonekana kama juhudi za kuimarisha ushawishi wake mashinani huku miungano mipya ikiendelea kusukwa. Katika ujumbe aliochapisha kwenye ukurasa wake wa mtandao wa X mnamo Ijumaa, Mei 29, 2026, Mbunge wa Suba Kusini Caroli Omondi alitoa ujumbe mfupi lakini uliosisimua wafuasi wa vuguvugu. “Tumerejea! Tupatane Machakos Jumapili Mei 31, 2026,” aliandika. Wachanganuzi wametafsiri tangazo hilo kama ishara ya kuongezeka kwa shughuli za kundi la Linda Mwananchi ambalo linaendelea kujipanga upya baada ya ODM kuachana rasmi na kaulimbiu ya “Linda Ground”. Machakos ambako mkutano huo utafanyika ni mojawapo ya ngome kuu za kisiasa za kiongozi wa Wiper, Kalonzo Musyoka, na eneo muhimu kwa muungano wa upinzani ambao unalenga kusuka ushirikiano na vuguvugu la Seneta Sifuna. Hatua hiyo inaonekana kuongeza uzito wa kisiasa wa mkutano huo huku vinara wa upinzani wakisaka njia mpya za kuunganisha nguvu dhidi ya utawala wa Rais William Ruto. Mkutano huo unatarajiwa kuvutia viongozi na wafuasi kutoka maeneo mbalimbali huku kampeni zikianza kushika kasi kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027. Tangazo la Omondi limejiri siku chache baada ya Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga kufichua kuwa ODM imeachana na kaulimbiu ya “Linda Ground” baada ya madai kwamba baadhi ya makundi yalikuwa yameanza kuipotosha kisiasa. Akizungumza katika mkutano wa mashauriano na wawaniaji wanaosaka tikiti ya ODM, mjini Kisumu mnamo Jumatatu, Gavana Wanga alisema wanachungwa sasa wanapaswa kutumia nembo na rangi rasmi za chama hicho pekee. “Tulikuwa tumeanzisha vuguvugu la Linda Ground ili kuimarisha msingi wetu wa kisiasa, lakini baadhi ya watu walikuja na mambo tofauti. Sasa tumeachana na hilo. Sisi ni ODM na rangi yetu ni chungwa,” alisema Wanga. Aidha, alisisitiza kuwa ODM bado imeungana chini ya uongozi wa Seneta wa Siaya Oburu Oginga licha ya pandashuka zinazoendelea ndani ya chama hicho cha chungwa. Ingawa ajenda rasmi ya mkutano wa Machakos bado haijawekwa wazi, mkutano huo tayari umechochea mjadala kuhusu uwezekano wa kuundwa kwa ushirikiano mpya wa kisiasa kati ya vinara wa upinzani na kundi la Linda Mwananchi. Kurejea kwa mikutano ya kisiasa mashinani na kuibuka kwa mirengo mipya kunaonyesha jinsi ushindani wa kisiasa unazidi kushika kasi nchini huku viongozi wakijipanga kwa kura ya mwaka ujao. Wakati huo huo, Gavana wa Siaya James Orengo ameapa kuwa vuguvugu la Linda Mwananchi halitatishwa baada ya mmoja wa wafuasi wake Evans “Kidero Jasuba” Kawala kukamatwa na baadaye kuachiliwa kwa dhamana. Katika taarifa yake ya Mei 28, 2026, Bw Orengo alisema timu ya mawakili iliyoongozwa na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino ilisaidia kuachiliwa kwa Kawala huku akisisitiza kuwa wanachama wa vuguvugu hilo waliendelea kuonyesha mshikamano. “Kama Linda Mwananchi, hatutakubali kurudi nyuma. Tulisimama bega kwa bega na Evans ‘Kidero Jasuba’ Kawala kufuatia kukamatwa kwake kwa misingi ya kisiasa,” alisema Bw Orengo. Pia aliwasifu wanachama wa mtandao wa Bunge la Wananchi kwa kujitokeza kwa wingi mahakamani kama ishara ya mshikamano. “Heshima kubwa kwa familia ya Bunge la Wananchi kwa kujitokeza na kusimama imara kwa mwenzao,” alisema. Awali, Bw Orengo alikuwa ameishutumu serikali kwa madai ya kumteka nyara Kawala kwa sababu ya kuikosoa serikali ya Rais Ruto. Kwa upande wake, DCI ilisema Kawala alikamatwa kutokana na matamshi ya uchochezi yaliyokuwa yakisambazwa kwenye mitandao ya kijamii. Katika taarifa yake ya Mei 27, 2026, DCI ilisema maudhui hayo yalionekana kuhatarisha mshikamano wa kitaifa pamoja na utulivu wa nchi.
May 31, 2026 at 06:55AM
KWA miongo kadhaa, Padre John Pesa I alikuwa mmoja wa viongozi wa kidini waliovutia hisia kali zaidi katika eneo la Nyanza. Wapo waliomchukulia kama mtumishi wa Mungu mwenye uwezo wa kipekee wa kiroho, huku wengine wakimwona kama mhusika wa utata ambaye mara kwa mara alijikuta akipingana na wanaharakati wa haki za kibinadamu na mamlaka za serikali. Alikuwa mtu ambaye uwepo wake haukuweza kupuuzwa. Mara nyingi alionekana akizungukwa na kundi la wafuasi waaminifu, walinzi wa kibinafsi waliovalia suti nyeusi na maafisa wa polisi waliokuwa wakimlinda kana kwamba alikuwa kiongozi wa taifa. Alipopita mitaani au kuhubiri mbele ya waumini, kila macho yalielekezwa kwake. Hivyo basi, habari za kifo chake zilipoanza kusambaa Alhamisi asubuhi, majonzi makubwa yaliwakumba wafuasi wake. Katika Mochari ya Kwee ndani ya Hospitali ya Rufaa na Mafunzo ya Jaramogi Oginga Odinga, huzuni ilitanda huku waumini wakikusanyika kwa makundi madogo, wakijaribu kukubaliana na ukweli kwamba kiongozi wao alikuwa ameaga dunia. Mwili wake uliripotiwa kufikishwa katika hospitali hiyo na viongozi wakuu wa kanisa baada ya kufariki. Awali ulipelekwa katika mochari kuu kabla ya kuhamishwa hadi Mochari ya Kwee. Kupitia kwa Mchungaji Kennedy Otieno, kanisa hilo lilikataa kutoa maelezo ya kina kuhusu kifo hicho, likisema taarifa rasmi ingetolewa baadaye kutokana na hadhi ya Padre Pesa ndani ya taasisi hiyo. Padre Pesa alijulikana zaidi kama mwanzilishi wa Kanisa la Holy Ghost Coptic Church of Africa lenye makao yake makuu eneo la Mamboleo, kando ya barabara ya Kisumu-Kakamega. Safari yake ilianza baada ya kutengwa na Kanisa Katoliki mwaka 1971. Tukio hilo lilimchochea kuanzisha dhehebu lake mwenyewe ambalo baadaye lilikua na kupata maelfu ya waumini katika maeneo mbalimbali ya nchi. Lakini pamoja na mafanikio hayo, jina lake liliendelea kuandamwa na utata. Mojawapo ya madai yaliyomletea ukosoaji mkubwa ni kwamba kanisa lake lilikuwa likiwahifadhi watu waliodaiwa kuwa na matatizo ya akili kwa lengo la kufanyiwa maombi ya uponyaji. Padre Pesa alisisitiza mara kwa mara kuwa watu waliokuwa wakifungwa minyororo katika kanisa lake walikuwa wale waliokuwa na tabia za vurugu na kwamba hatua hiyo ilikuwa ya kuwalinda wao wenyewe pamoja na watu waliowazunguka. Hata hivyo, wanaharakati wa haki za kibinadamu walihoji utaratibu huo. Ripoti moja ilidai kuwa baadhi ya wagonjwa walikuwa wakifungiwa katika mazingira yasiyoridhisha, kunyimwa huduma muhimu na kutengwa kwa muda mrefu. Mwaka 2023, alifikishwa mahakamani kwa madai ya kuwahifadhi watu 23 wenye matatizo ya akili katika mazingira yasiyofaa. Lakini baadaye alipata ushindi wa kisheria baada ya mahakama kutupilia mbali kesi iliyotaka kanisa lake libomolewe kutokana na madai hayo. Baada ya ushindi huo, Padre Pesa alieleza kuwa madai dhidi yake yalikuwa njama za kumchafua jina na alisisitiza kuwa hakuna mtu aliyekuwa akizuiliwa dhidi ya mapenzi yake na kwamba familia za waathiriwa zilikuwa zikitia saini fomu za idhini kabla ya kuwapeleka katika kanisa hilo. Mwaka huohuo, kamati maalumu iliyokuwa ikichunguza kuongezeka kwa makanisa yenye utata nchini ilitembelea kanisa lake. Wanachama wa kamati hiyo walieleza wasiwasi kuhusu hali ya makazi ya baadhi ya watu waliokuwa wakisubiri kuombewa. Kamati hiyo hata ilifananisha eneo hilo na “Shakahola ndogo” na kuwaokoa watu kadhaa waliokuwa humo. Mbali na masuala ya dini, Padre Pesa pia alihusishwa mara kwa mara na mijadala kuhusu ajali zilizokuwa zikitokea karibu na Mzunguko wa Coptic ulio karibu na kanisa lake. Baadhi ya wakazi waliamini kuwa misafara yake ya kidini ilihusishwa kwa njia fulani na ajali katika eneo hilo. Hata hivyo, uchunguzi uliofanywa baadaye ulionyesha kuwa changamoto kubwa ilikuwa usanifu mbovu wa barabara. Hatimaye, Mamlaka ya Kitaifa ya Barabara Kuu Kenya (KeNHA) ilitangaza mpango wa kuubadilisha mzunguko huo ili kupunguza ajali. Katika siasa, Padre Pesa alikuwa tofauti na viongozi wengi wa kidini kutoka Nyanza waliokuwa wakiegemea upande wa upinzani. Yeye alijulikana kwa kushirikiana na serikali iliyokuwa mamlakani bila kujali chama kilichokuwa madarakani. Katika ofisi yake kulining’inia picha zake akiwa pamoja na marais wote wa Kenya kuanzia Jomo Kenyatta, Daniel arap Moi, Mwai Kibaki, Uhuru Kenyatta hadi William Ruto. Alijulikana pia kwa ucheshi wake. Kauli yake maarufu zaidi iliyosambaa mitandaoni ni pale alipodai kuwa Mfalme Sulemani ndiye aliyemuua Goliathi badala ya Daudi, jambo lililozua vicheko na mjadala mkubwa. Kwa wanahabari waliomtembelea mara kwa mara, alikuwa na desturi ya kuwakaribisha kwa chupa ya soda ya mililita 500 na tabasamu pana usoni. Kwa Padre Pesa, umaarufu haukuwa mzigo. Habari zote zilizomhusu, iwe ni sifa au ukosoaji, zilikuwa zikibandikwa katika ubao wa matangazo ndani ya ofisi yake kama kumbukumbu za maisha yaliyojaa matukio.
May 31, 2026 at 05:55AM
VIONGOZI mbalimbali wa kisiasa na kijamii wamejitokeza kumtetea Katibu Mkuu wa UDA, Hassan Omar, kufuatia wito wa baadhi ya watu kutaka ajiuzulu kutoka wadhifa wake. Akizungumza katika mkutano na wanahabari, Bw Said Twaha alisema kuwa kauli ya Bw Omar kuhusu ardhi ilitafsiriwa vibaya. Alieleza kwamba Katibu huyo hakumaanisha kuchukua ardhi ya watu, bali alisisitiza kuwa ardhi iliyonyakuliwa isivyo halali inapaswa kurejeshwa kwa wamiliki wake wa awali . "Sisi tuko nyuma ya Bw Sarai, na wanataka ajiuzulu ni wakabila wanataka kuchukua nafasi hiyo iliyotengewa watu wa Pwani," alisema Bw Twaha. Kwa upande wake, kiongozi wa vijana Suleiman Hassan alisema hakuna sababu ya Bw Omar kujiuzulu. Alibainisha kuwa nafasi mbalimbali ndani ya chama zilitolewa kwa kuzingatia uwiano wa kikanda ili kuhakikisha kila eneo la nchi linawakilishwa ipasavyo. Naye Mohammed Jere, ambaye ni kiongozi katika jamii ya Wasomali, alisisitiza kuwa Hassan Omar amekuwa kiungo muhimu katika chama hicho. Alionya kuwa kuondolewa kwake kunaweza kusababisha baadhi ya wanachama kutoka jamii ya Wasomali kukipuuza au hata kukihama chama cha UDA. "Viongozi hao pia wanaotaka Bw Omar aondolewe madarakani, wakisema kuwa hoja zao zinaegemea ukabila badala ya masuala ya utendaji kazi. Si vyema kutumia tofauti za kikabila kama msingi wa kufanya maamuzi ya kisiasa," alisema Bw Jere. Kwa upande wake, Francis Maina alisema Kenya inapaswa kuendelea kuimarisha umoja wa kitaifa na kuepuka siasa za ukabila. Alisisitiza kuwa viongozi wanapaswa kuhukumiwa kwa misingi ya utendaji wao na si kwa asili au jamii wanayotoka. Viongozi hao walitoa wito kwa wanachama wa UDA kuendelea kumuunga mkono Bw Omar na kudumisha mshikamano ndani ya chama.  
May 31, 2026 at 04:55AM
KWA miaka mingi, Ruth Odinga alisalia kivulini mwa kakake marehemu Raila Odinga, mwanasiasa aliyekuwa nguzo ya upinzani nchini kwa miongo kadhaa hadi alipofariki Oktoba 2025. Hata hivyo, nyuma ya pazia, Ruth amekuwa mmoja wa viongozi wa kudumu ndani ya Orange Democratic Movement tangu kuanzishwa kwake takriban miaka 20 iliyopita. Kabla ya kuingia katika siasa za uchaguzi mwaka 2013 kama Naibu Gavana wa Kisumu, alikuwa akiongoza kampuni ya Spectre International, inayomilikiwa na familia ya Odinga. Sasa akiwa Naibu Katibu wa Uhamasishaji wa ODM, Ruth amejikuta katikati ya mzozo unaotikisa chama hicho kufuatia kifo cha Raila. Katika mahojiano na Taifa Jumapili, alisema kinachomsumbua zaidi si mashambulizi ya kisiasa anayopokea kutoka kwa Waziri wa Fedha John Mbadi, bali hatari ya ODM kusambaratika kutokana na migawanyiko ya ndani. Kwa mujibu wake, msimamo wake umekuwa mmoja tu: chama lazima kibaki kimeungana. “Nilichosema katika mkutano wa Mombasa ni kwamba ODM inapaswa kubaki imara na yenye umoja ili iweze kusimamisha mgombea wake wa urais au kujadiliana kutoka nafasi ya nguvu katika miungano ya baadaye ya kisiasa. Huo ndio ulikuwa mtazamo wa Raila,” alisema. Ruth alisema alishangazwa na shutuma alizorushiwa baada ya kutoa wito wa umoja, akidai baadhi ya viongozi wanaonekana kutafsiri kauli hiyo kama kuunga mkono upande fulani. Alisema mashambulizi ya Mbadi dhidi yake na dhidi ya binti ya Raila, Winnie Odinga, hayakuwa ya lazima. “ODM daima imekuwa chama kinachowapa vijana nafasi ya kujieleza. Winnie alizungumza yale ambayo vijana wengi wanahisi kuhusu uongozi na mustakabali wa chama,” alisema. Ruth alisema alitarajia Mbadi, ambaye mara nyingi husema Raila alimlea kisiasa, angeonyesha uvumilivu na kumwelekeza Winnie badala ya kupuuza maoni yake. Akizungumzia mivutano ndani ya ODM, alisema kuna wakati mtu hujiuliza kama kuna maslahi mengine yanayochochea migawanyiko hiyo. Kwa sasa chama kimegawanyika katika makundi mawili makuu; kundi linalohusishwa na kiongozi wa chama Oburu Oginga ambalo hapo awali lilijulikana kama “Linda Ground”, na lile la Katibu Mkuu Edwin Sifuna linalojulikana kama “Linda Mwananchi”. “Kauli mbiu yetu inapaswa kubaki Chungwa Moja, Maisha Bora. ODM ilifanikiwa kwa sababu iliunganisha watu wa makabila, vizazi na mitazamo tofauti chini ya mwavuli mmoja,” alisema. Kuhusu jina la Odinga katika siasa, Ruth alisema wengi hudhani limekuwa chanzo cha manufaa, lakini husahau gharama kubwa ambayo familia hiyo imelipa. Alikumbuka jinsi familia yao ilivyokumbwa na mateso ya kisiasa kutokana na shughuli za baba yao, Jaramogi Oginga Odinga, aliyekuwa mmoja wa viongozi wakuu wa mapambano ya demokrasia nchini. Baada ya jaribio la mapinduzi ya mwaka 1982, alisema alilazimika kuishi uhamishoni katika Uganda, Tanzania na Zimbabwe kabla ya kwenda kusoma nchini Norway. “Maisha hayo yalinifundisha uvumilivu na kuimarisha imani yangu katika demokrasia na haki,” alisema. Ruth pia alikataa madai kwamba ODM imekuwa chama kinachozunguka mtu mmoja badala ya taasisi. Alisema historia ya chama hicho ilijengwa kupitia ushiriki wa wananchi wa kawaida tangu enzi za FORD, NDP, NARC hadi kuzaliwa kwa ODM. “ODM ni kubwa kuliko mtu yeyote mmoja. Nguvu zake zimekuwa katika kujumuisha kila mtu na kusikiliza maoni tofauti,” alisema. Kuhusu uchaguzi mkuu ujao, alisema chama kinapaswa kushauriana kwa upana kabla ya kuamua kama kitasimamisha mgombea wake wa urais au kuunga mkono mpangilio mwingine wa kisiasa. Lakini jambo analosisitiza zaidi ni maridhiano kati ya makundi yanayopingana. “Ninaamini kabisa maridhiano yanawezekana. Nimeona migogoro mikubwa zaidi ikitatuliwa kupitia mazungumzo,” alisema, akirejelea ushiriki wake katika juhudi za kidiplomasia baada ya ghasia za baada ya uchaguzi wa 2007. Kwa maoni yake, migogoro ya sasa ndani ya ODM ni midogo ikilinganishwa na changamoto ambazo chama na nchi zimewahi kupitia hapo awali. Alitoa wito kwa viongozi wa chama kuwapa nafasi vijana kama Sifuna, Babu Owino na Winnie Odinga, akisema wao ni sehemu muhimu ya kizazi kitakachobeba chama siku zijazo. Akizungumzia maisha baada ya kifo cha Raila, Ruth alisema bado hajapona kutokana na majonzi ya kumpoteza kaka yake pamoja na dada yao Beryl Achieng ndani ya kipindi kifupi. “Raila alifanyia Kenya mengi. Mchango wake kwa demokrasia na haki haupaswi kusahaulika. Bado sijakubali kikamilifu hasara hiyo,” alisema. Kwa sasa, anasema lengo lake kuu ni kuona ODM ikinusurika kipindi hiki kigumu cha mpito. “ODM lazima iokolewe. Tofauti za maoni zipo katika siasa, lakini chama makini hutatua migogoro yake kupitia mazungumzo, si kupitia vita hadharani,” alisema.
May 31, 2026 at 03:55AM
MAONI ya umma katika mitandao ya kijamii kuhusu Mswada wa Fedha 2026 umekuwa hasi kwa kiwango kikubwa, huku mijadala mingi ikitawaliwa na alama ya #RejectFinanceBill2026, kwa mujibu wa uchambuzi wa machapisho 3,000 kwenye X yaliyochapishwa kati ya Mei 2 na Mei 26. Watumiaji wengi wa mitandao ya kijamii wametaja mswada huo kama unaolenga kuwakandamiza wananchi, na kuongeza mzigo wa kiuchumi. Ni sehemu ndogo tu ya machapisho yaliyoonyesha mswada huo unaungwa mkono, huku hata mijadala isiyo na msimamo ikijikita zaidi katika kuhoji vifungu au kufanya uhakiki wa taarifa badala ya kuunga mkono sheria hiyo. Masuala matatu yameibuka kuwa chanzo kikuu cha hasira mtandaoni: kuongezwa kwa mamlaka ya Mamlaka KRA, mapendekezo ya kutoza kodi kwenye majukwaa ya malipo ya kidijitali, na mkanganyiko kuhusu ushuru wa simu za kisasa. Katika suala la KRA, pendekezo linaloruhusu mamlaka hiyo kutumia taarifa zilizokusanywa kutoka kwa taasisi za kifedha na makampuni ya mawasiliano kukadiria mapato ya walipa ushuru limeibua hofu kubwa. Wataalamu wa ushuru wanasema hatua hiyo inaweza kuhamisha mzigo wa kwa mlipa ushuru, ambapo mtu atapaswa kuthibitisha kuwa makadirio ya KRA si sahihi badala ya KRA kueleza jinsi ilivyofikia hesabu hizo. Wataalamu pia wameeleza wasiwasi kuhusu ukosefu wa uwazi katika mfumo huo. Suala jingine linalojadiliwa kwa mapana ni pendekezo la kutoza ushuru wa ongezeko la thamani (VAT) wa asilimia 16 kwa majukwaa ya malipo ya kidijitali kama M-Pesa, Airtel Money na Pesapal. Wizara ya Fedha imetetea pendekezo hilo ikisema VAT inapaswa kutozwa kwa watoa huduma za ICT wanaowezesha miamala. Hata hivyo, wachambuzi wanaonya kuwa gharama hizo zinaweza kuhamishiwa kwa watumiaji kupitia ada za juu za miamala, jambo litakalowaathiri zaidi wananchi wa kipato cha chini wanaotegemea huduma hizo. Mswada huo pia umeleta mkanganyiko kuhusu mabadiliko ya ushuru wa simu za kisasa.   Waziri John Mbadi amesema serikali inalenga kupunguza mzigo wa ushuru kwa simu kutoka asilimia 55 hadi asilimia 25 kupitia kuunganisha uliopo kwa sasa. Hata hivyo, wananchi wengi mitandaoni bado hawajaridhika, wakisema maelezo ya serikali si wazi na yanaweza kupotosha kuhusu gharama halisi za simu sokoni. Mbali na hoja za sera, mtandao umegeuka uwanja wa mapambano ya taarifa sahihi na potofu. Baadhi ya mitandao imeeneza madai ya uongo kwamba mswada huo unaanzisha ushuru mpya kwa bidhaa za msingi kama mkate, madai ambayo hayamo kwenye sheria hiyo. Kukabiliana na hilo, baadhi ya watumiaji wameanzisha kampeni za kurekebisha taarifa hizo na kuhimiza uhakiki wa taarifa kabla ya kusambazwa. Alama ya reli ya #FB2026Facts imeibuka kama juhudi ya kupinga upotoshaji, huku zaidi ya machapisho 170 yakitumiwa kubaini na kupinga taarifa zisizo sahihi. Wakati huo huo, kampeni nyingine ya kuunga mkono mswada ambapo zaidi ya machapisho 1,400 yanaonekana kusambaza ujumbe unaofanana, hali inayoashiria kampeni iliyoratibiwa badala ya mazungumzo ya kawaida ya wananchi. Kwa ujumla, Mswada wa Fedha 2026 umeibua si tu upinzani mkubwa mtandaoni, bali pia mazingira ya taarifa ambapo hoja za wananchi, propaganda na upotoshaji vinachangia kwa kiasi kikubwa kuunda mtazamo wa umma kwa wakati halisi.
May 31, 2026 at 02:55AM
UPINZANI dhidi ya mpango kati ya Serikali ya Kenya na Amerika wa kuanzisha kituo cha kutenga wagonjwa wa Ebola katika Kaunti ya Laikipia umeanza kushika kasi, baada ya viongozi wa eneo hilo, madaktari na mashirika ya kiraia kuungana kupinga utekelezaji wake. Wakenya wanasema mpango huo haujafafanuliwa kikamilifu kwa wananchi na unaibua maswali mazito ya kiusalama na kisera. Mahakama Kuu tayari imesitisha utekelezaji wa mpango huo kufuatia kesi iliyowasilishwa na Katiba Institute, hatua iliyopokelewa kwa furaha na viongozi wa Laikipia na baadhi ya makundi ya kisiasa nchini. Kwa mujibu wa taarifa zinazoendelea kujadiliwa nchini, Amerika inapanga kuanzisha kituo cha vitanda 50 katika Laikipia, Nanyuki, ambacho kitatumika kutenga raia wake walio katika hatari ya maambukizi ya Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC). Kituo hicho kitasimamiwa na maafisa wa afya wa Amerika na kuwa na wataalamu takribani 30 kutoka Huduma ya Afya ya Umma ya Amerika. Hata hivyo, mpango huo umekumbana na upinzani mkali kutoka kwa Wakenya, ambao wanasema unaleta hatari ya kugeuza nchi kuwa kituo cha kuhifadhi wagonjwa wa nje huku mfumo wa afya wa ndani ukiwa bado dhaifu. Viongozi wa Laikipia Mbunge wa Laikipia Mashariki Mwangi Kiunjuri, wenzake wa Laikipia Magharibi Wachira Karani, Sarah Korere wa Laikipia Kaskazini na Mwakilishi wa Kike Jane Kagiri walisema kwa pamoja kuwa, hawakubaliani na mpango huo, wakisisitiza kuwa haujazingatia maslahi ya wananchi wa eneo hilo wala usalama wa taifa. “Kwa mtazamo wetu kama wawakilishi wa wananchi wa Laikipia, tunaona hakuna mantiki kwa kaunti yetu kuwa eneo la kituo cha Ebola. Serikali lazima iwe wazi kwa wananchi kuhusu makubaliano haya na kwa nini Laikipia imechaguliwa,” walisema katika taarifa yao ya pamoja. Viongozi hao walihoji pia kwa nini Amerika haijaweka kipaumbele kuanzisha kituo hicho katika eneo la mlipuko wa ugonjwa huo, hasa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, badala ya kusafirisha raia wake kwenda nchi ya tatu. Walisema hatua hiyo inaibua maswali ya kimaadili na kiusalama kuhusu uwajibikaji wa kimataifa katika udhibiti wa magonjwa hatari. Walisema pia wananchi wa Laikipia wanastahili kulindwa na serikali yao na si kuwa sehemu ya majaribio ya mipango ya kimataifa isiyoeleweka vizuri. Jana, Chama cha Madaktari, Wafamasia na Madaktari wa Meno (KMPDU) kilitoa onyo kali kikisema Kenya haijajiandaa kikamilifu kukabiliana na mlipuko wa Ebola iwapo utatokea. Katibu Mkuu wa KMPDU, Davji Atellah, alisema mfumo wa afya nchini bado unakabiliwa na changamoto kubwa za uhaba wa watumishi, ukosefu wa vifaa vya kisasa na vitengo duni vya wagonjwa mahututi (ICU), hali inayofanya taifa kuwa katika hatari kubwa iwapo ugonjwa huo utaingia. “Je, serikali imeweka mipango gani kwa Wakenya? Je, wahudumu wa afya wamefundishwa? Je, ICU ziko tayari? Hatupaswi kuanza kujadili makubaliano na wageni wakati Wakenya wenyewe hawana huduma bora za afya,” alisema Atellah. Aliongeza kuwa serikali inapaswa kwanza kuimarisha hospitali, kuajiri madaktari waliokosa ajira na kuwekeza katika vifaa vya matibabu kabla ya kufikiria makubaliano ya kuanzisha vituo vya karantini kwa raia wa kigeni. KMPDU ilisisitiza kuwa, njia bora ya kupambana na Ebola ni kuimarisha juhudi za kudhibiti ugonjwa huo katika chanzo chake, hasa DRC, ambako maambukizi yanaendelea kuripotiwa kutokana na changamoto za usalama na miundombinu. Mahakama Kuu ilipotoa amri ya kusitisha mpango huo, ilieleza kuwa kesi hiyo inahusisha masuala mazito ya kikatiba yanayohusu afya, ushiriki wa umma na usalama wa taifa. Uamuzi huo ulifungua mlango wa mjadala mpana zaidi kuhusu uwazi wa mikataba ya kimataifa inayoathiri afya ya wananchi. Wakati huo huo, baadhi ya maafisa wa serikali ya Amerika wameripotiwa kuonyesha matumaini kwamba, mzozo huo unaweza kutatuliwa kupitia mazungumzo na serikali ya Kenya. Hata hivyo, upande wa Kenya haujatoa maelezo rasmi ya kina kuhusu makubaliano hayo, hali iliyoongeza taharuki miongoni mwa wananchi. Wakenya mitandaoni walikataa mpango unaopendekezwa wa kituo cha karantini ya Ebola mjini Nanyuki, kaunti ya Laikipia. Wengi wameeleza hofu ya usalama wakitaka serikali itoe maelezo ya wazi kabla ya kukubali mpango huo. Mmoja wa watumiaji wa X aliandika: “Hatukatai msaada wa kimataifa, lakini kwa nini Laikipia na kwa nini Kenya wakati ugonjwa uko Congo?” Mwingine alisema: “Afya yetu sio majaribio ya kisiasa. Serikali itueleze ukweli wa haya makubaliano na Amerika.” Kwenye Facebook, baadhi ya maoni yalikuwa makali zaidi, yakilenga uwazi wa serikali. Mchangiaji mmoja aliandika: “Kama Amerika wanaogopa kupeleka wagonjwa wao nyumbani, sisi tunakubali kwa nini? Hii ni hatari kwa wananchi.” Wengine walikosoa miundombinu ya afya nchini wakisema mfumo hauko tayari. Mtumiaji mmoja alisema: “Hatutakuwa na ICU za kutosha, halafu tunaleta Ebola? Hii ni kutupeleka mautini.” Hata hivyo, wapo wachache waliotetea mpango huo wakisema ni sehemu ya ushirikiano wa kimataifa. Mmoja aliandika: “Kama kutakuwa na ufuatiliaji mkali wa afya, ushirikiano huu unaweza kuwa na manufaa. Mjadala huo unaendelea kushika kasi mtandaoni huku #RejectEbolaFacility na nyingine zikisambaa kuonyesha jinsi suala hilo lilivyoibua wasiwasi mkubwa kitaifa .

To continue using the website, you must be logged in.

Your login information is stored on your browser only.

OR

Support Our Website

Ads help us keep our content on kenyalivetv.co.ke free for you. Please consider supporting us by disabling your ad blocker or whitelisting our site in your ad blocker settings.

You are currently offline.
You are back online.