May 11, 2026 at 05:51PM
UHASAMA wa kisiasa unazidi kutokota kati ya Jubilee na DCP baada ya vyama hivyo viwili kusema vitakuwa na mgombeaji kwenye uchaguzi mdogo wa Ol Kalou.
Baada ya DCP kuandaa mchujo wake, sasa ni dhahiri kuwa chama hicho kitakuwa na mgombeaji na hakutakuwa na ushirikiano wa kisiasa upinzani jinsi ilivyokuwa katika kura ya Mbeere Kaskazini mnamo Novemba mwaka jana.
Aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua analenga kutumia uchaguzi huo mdogo kuonyesha kuwa ndiye kigogo wa siasa za Mlima Kenya.
Kwa upande mwingine Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta ambaye ni kiongozi wa Jubilee, ametangaza kuwa anamuunga mkono Dkt Fred Matiangí kwa urais mnamo 2027 na analenga kudhihirisha kuwa licha ya kuondoka mamlakani, bado ana ushawishi kisiasa eneo la Mlima Kenya.
Kwa mujibu wa mbunge wa zamani wa Starehe Maina Kamanda, Jubilee lazima ijifunze kuwa upinzani utaendelea kuungana tu iwapo mbinu za kushinda viti zitakumbatiwa badala ya ubabe wa kisiasa.
“Sisi ni miungano ya vyama mbalimbali na lazima tujue kuwa ngome ya kila chama ndiyo itaamue unapata nini kwenye muafaka wa upinzani,” akasema.
Bw Kamanda ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Viongozi wakongwe wa kutoa ushauri ndani ya DCP.
Alimtaka Dkt Matiangí amakinikie kuunganisha ngome yake ya Gusii badala ya kushinda na DCP Mlimani.
“Mnamo 20022, marehemu Simeon Nyachache alichukua chama cha Ford People ambacho kilikuwa na asili yake Mlima Kenya kutoka kwa Kimani wa Nyoike na kukifanya kuwa maarufu Gusii. Dkt Matiangí anastahili kufuata mkondo huo na kuhakikisha Jubilee inajizolea umaarufu wake Gusii,” akasema Bw Kamanda.
May 11, 2026 at 03:56PM
KINARA wa Mawaziri Musalia Mudavadi ameonyesha imani yake kuwa Rais William Ruto atashinda 2027 kwa zaidi ya asilimia 70.
Akiongea kwenye mahojiano na kituo kimoja nchini Jumatatu, Mei 11, 2026, Mudavadi alisema wataendesha kampeni kali ambayo itahakikisha rais anashinda kwa kura nyingi kiasi kuwa upinzani hata utaaibika kuelekea kortini.
Alisema pengo kubwa la ushindi litaonyesha kuwa umma una imani na utendakazi wa serikali ya Kenya Kwanza.
Bw Mudavadi alisema kuwa kumekuwa na kesi za kupinga matokeo ya urais kwa sababu ya mwanya mdogo wa ushindi kati ya wawaniaji wakuu wa urais.
May 11, 2026 at 03:31PM
May 11, 2026 at 02:49PM
TUNAPOTUNGA sentensi sharti tuzingatie upatanisho wa kisarufi ili sentensi ziwe sahihi.
Upatanisho wa kisarufi katika sentensi hutokana na jinsi nomino huathiri vitenzi katika sentensi. Kila kundi la nomino huwa na viambishi vyake vya upatanisho wa kisarufi.
Watu wengi wanaowasiliana kwa lugha ya Kiswahili hasa wanafunzi huzingatia upatanisho sahihi wa kisarufi wanapotunga sentensi, japo baadhi yao hukumbwa na changamoto.
Utapata sentensi kama vile:
* Nchi nyingi barani Afrika wanahimiza umoja na amani.
* Vyombo vya habari wapeperusha taarifa kuhusu wahalifu waliokamatwa jana.
* Jamii yetu wanazingatia maadili.
Mifano hii ya sentensi imetumia viambishi vya upatanisho wa kisarufi visivyofaa.
Kosa hilo hasa linatokana na kukosa kuzingatia kiambishi ngeli cha nomino iliyotumiwa kutunga sentensi.
Katika sentensi ya kwanza, kiambishi wa- kimetumiwa kuwakilisha nomino nchi.
Hili ni kosa kwani ingawa nchi zina watu ambao ndio wanahimiza umoja na amani, nomino iliyotumiwa kutunga sentensi ni nchi, kwa hivyo tunafaa kutumia kiwakilishi ngeli cha nomino nchi si nomino watu.
Ili kusahihisha sentensi hizo tunafaa kusema: Nchi nyingi barani Afrika zinahimiza umoja na amani.
Vyombo vya habari vipeperusha taarifa kuhusu wahalifu waliokamatwa na polisi jana. Jamii yetu inazingatia maadili.
Mwanafunzi anayekumbwa na changamoto ya kutotumia viambishi sahihi vya upatanisho wa kisarufi katika sentensi, afanye mazoezi ya kutambua nomino katika ngeli mbalimbali.
Atambue viambishi sahihi vya upatanisho wa kisarufi katika kila ngeli kisha atumie nomino katika ngeli mbalimbali kutunga sentensi zenye upatanisho sahihi wa kisarufi.
May 11, 2026 at 02:46PM
KAUNTI ya Laikipia ikiwa miongoni mwa maeneo ambayo athari za tabianchi zinaendelea kutatiza mifumo ya jadi ya ufugaji, mabadiliko makubwa yanaibuka kimya kimya yakiongozwa na ngamia na wanawake.
Kati ya wanaofanikisha mageuzi hayo ni kampuni ya White Gold Camel Milk Limited, biashara inayokua kwa kasi na kubadilisha maziwa ya ngamia kuwa chanzo cha mapato, lishe bora na uthabiti kwa jamii za wafugaji.
Kampuni hiyo ilianzishwa na Zamzam Haji, ambaye huchakata na kuuza bidhaa za maziwa ya ngamia kwa wateja mbalimbali wanaoongezeka kila siku. Kutoka familia za mijini zinazotafuta njia mbadala yenye afya ya maziwa ya kawaida hadi watu wenye matatizo ya lactose, kisukari na wazee, bidhaa za White Gold Camel Milk zimeanza kujitokeza kwenye soko lenye ushindani mkuu nchini, la maziwa.
Bidhaa zake ni pamoja na maziwa halisi ya ngamia, brandi ya vanilla na strawberry, pamoja na maziwa yaliyogandishwa yanayojulikana kama “susa” katika jamii za wafugaji – somali. Bidhaa hizo sasa zinapatikana katika baadhi ya maduka makubwa nchini huku kampuni hiyo pia ikitoa huduma kusambazia wateja bidhaa nyumbani.
“Ni kampuni inayonufaisha zaidi wanawake, hasa wanawake kutoka jamii za wafugaji ambao kwa muda mrefu hawakuwa na masoko rasmi ya kuuza maziwa yao,” Zamzam anasema.
[caption id="attachment_187951" align="aligncenter" width="300"] Zamzam Haji, mwanzilishi White Gold Camel Milk Limited Kaunti ya Laikipia. Picha|Sammy Waweru[/caption]
Leo hii, wanawake wanawakilisha karibu asilimia 80 ya wasambazaji wa maziwa kwa kampuni hiyo. Wengi wao, Zamzam anasema maziwa ya ngamia si bidhaa tu ya matumizi nyumbani bali ni njia ya kujitegemea kifedha, kujiendeleza kimaisha na kupata heshima katika jamii.
Mama huyu anasema safari ya kuanzisha biashara hiyo ilianza mwaka 2017 baada ya kubaini pengo kubwa katika mnyororo wa thamani wa maziwa eneo la Laikipia.
“Wanawake wengi walikuwa na ngamia na walizalisha maziwa mengi, lakini hawakuwa na mnunuzi wa kutegemewa baada ya kampuni moja kufungwa,” anakumbuka.
Kwa kushirikiana na mumewe aliyekuwa akiishi nchini Amerika wakati huo, walianzisha kiwanda kidogo kwa kutumia akiba yao binafsi na fedha walizokopa kutoka kwa familia kwa sababu hawangeweza kupata mikopo rasmi kutoka kwa benki au mashirika ya kukopesha pesa.
Safari ilianza kwa kuchakata lita 50 pekee za maziwa kwa siku. Leo hii, karibu miaka 10 baadaye, kampuni hiyo huchakata hadi lita 300 kwa siku msimu wa mvua, ingawa kiwango hicho hupungua wakati wa ukame.
Zamzam, aliyelelewa katika jamii iliyotengwa ambapo wanawake walikuwa na nafasi finyu za maendeleo, anasema alitaka sana kujenga biashara inayoinua wanawake katika kila hatua ya uzalishaji.
[caption id="attachment_187952" align="aligncenter" width="300"] Zamzam Haji, mwanzilishi White Gold Camel Milk Limited Kaunti ya Laikipia wakati wa mahojiano Jijini Nairobi. Picha|Sammy Waweru[/caption]
Jitihada zake sasa zinaonekana wazi. Wanawake waliokuwa wakikosa soko la maziwa yao sasa wanapata kipato cha kudumu. Baadhi yao, Zamzam anaambia Akilimali kwamba wameweza hata kununua ardhi, jambo ambalo hapo awali lilikuwa ndoto kwa wanawake wengi.
Wakati huohuo, biashara hiyo imechangia mabadiliko katika ufugaji huku wafugaji wengi wakihamia ufugaji wa ngamia kutokana na ukame wa mara kwa mara. “Tofauti na ng’ombe, ngamia wanaweza kustahimili mazingira magumu na kuendelea kutoa maziwa hata wakati wa kiangazi,” anasema.
Licha ya mafanikio hayo, Zamzam anasema changamoto bado zipo, ikiwemo; ukosefu wa fedha kupanua biashara, kuelimisha wateja kuhusu maziwa ya ngamia, ushindani mkuu sokoni na ongezeko la wizi wa mifugo katika maeneo jirani kama vile Kaunti ya Isiolo.
Hata hivyo, Zamzam ana matumaini makubwa. Kampuni hiyo sasa inalenga masoko ya kimataifa hususan katika mataifa ya Uarabuni (Gulf).
Aidha, alikuwa miongoni mwa wafanyabiashara, kampuni na wajasiriamali walionufaika kupitia Farm’Innov acceleration programme, mpango uliozinduliwa mwaka 2024 kusaidia ubunifu na ushindani katika sekta ya kilimo na mifugo. Mpango huo wa mwaka mmoja ulifadhiliwa kupitia ushirikiano wa serikali ya Ufaransa na ile ya Kenya.
Kwa sasa, White Gold Camel Milk inamiliki ngamia 23 na inaendelea kufanya kazi na mtandao mkubwa wa wasambazaji wa maziwa – wengi wao wakiwa wanawake kutoka Laikipia na kaunti jirani.
May 11, 2026 at 01:11PM
MANCHESTER City inaendelea kujipa imani katika mbio za kufukuzia ubingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) msimu huu licha ya washindani wao wakuu Arsenal kufungua mwanya wa alama tano juu ya jedwali.
The Citizens walikuwa wamepunguza pengo hadi alama mbili dhidi ya vinara Arsenal Jumamosi walipoibamiza Brentford 3-0 ugani Etihad.
Kikosi cha kocha Pep Guardiola kilikuwa kimeteleza Jumatatu iliyopita kwa sare ya 3-3 dhidi ya Everton, lakini wikendi hii kilijikakamua kipindi cha pili na kuwapa mashabiki wao kila sababu ya kutabasamu.
Hata hivyo, furaha yao ilidumu kwa saa 24 pekee kwa sababu The Gunners walijinyakulia ushindi mwembamba na uliosheheni gumzo kubwa dhidi ya West Ham, pale goli la kusawazisha la The Hammers lilipokataliwa na VAR na kuruhusu vijana wa Mikel Arteta kuondoka na alama zote tatu.
Jumamosi huko Etihadi, nyota wa Ubelgiji Jeremy Doku alikuwa mwiba kwa difensi ya Brentford tangu mwanzo wa mchezo.
Alikosa bao la mapema baada ya kipa Caoimhin Kelleher kuokoa shuti lake, huku pia akimpakulia krosi safi Erling Haaland ambaye alikosa kulenga shabaha.
City walitawala kipindi cha kwanza lakini wakashindwa kuvunja ukuta wa Brentford. Baadaye Haaland alipiga kichwa kilichookolewa na Kelleher kabla ya juhudi nyingine kuzuiwa na Kristoffer Ajer.
Bao la kwanza liliwadia katika dakika ya 60 wakati Doku alipopenya upande wa kushoto na kupiga shuti kali lililotinga kona ya mbali.
Haaland aliongeza la pili dakika ya 75 baada ya vurugu ndani ya eneo la hatari, huku mchezaji wa akiba Omar Marmoush akifunga la tatu katika dakika za mwisho za kipindi cha pili.
Hata hivyo, Brentford pia walikuwa mwiba katika nyakati tofauti. Kipa Gianluigi Donnarumma alilazimika kufanya kazi ya ziada kuokoa mashambulizi ya Michael Kayode na Igor Thiago.
Baada ya ushindi huo, Guardiola alisema siri ya mabao ni kuwapeleka wachezaji karibu na Haaland.
Sasa City wanaomba sana Arsenal iteleze katika mechi zilizosalia na wao washinde zao dhidi ya Crystal Palace na Bournemouth ili mbio za ubingwa ziende hadi siku ya mwisho.
Kwingineko
Katika mechi nyingine, Liverpool walilazimishwa sare ya 1-1 katika mtanange uliogaragazwa nyumbani Anfield. Ryan Gravenberch alifungia wenyeji bao mapema dakika ya sita kabla ya Enzo Fernandez kusawazishia Chelsea dakika ya 35.
Mashabiki wa Liverpool walionyesha kutoridhishwa na maamuzi ya kocha Arne Slot, hasa baada ya kumtoa kinda Rio Ngumoha kipindi cha pili.
Nao Bournemouth waliibuka na ushindi muhimu wa 1-0 dhidi ya Fulham kupitia bao la la Rayan Christie dakika ya 53, katika mechi ya vuta nikuvute iliyoshuhudia kila timu ikibaki na wachezaji 10 kufuatia kadi nyekundu za kipindi cha kwanza baada ya ukaguzi wa VAR.
Rayan Rocha alikuwa wa kwanza kutimuliwa uwanjani baada ya kuonekana kumchezea vibaya Timothy Castagne katika tukio lililothibitishwa na VAR.
Hata hivyo, Fulham nao hawakudumu na idadi kamili ya wachezaji baada ya beki Joachim Andersen kupewa kadi nyekundu kwa kosa kama hilo dhidi ya Adrien Truffert.
Ushindi huo umeimarisha matumaini ya Bournemouth kumaliza msimu katika nafasi za kushiriki michuano ya Uropa msimu ujao.
Katika mtanange mwingine, Brighton waliwanyorosha washika mkia Wolves 3-0 na kupanda hadi nafasi ya saba kwenye jedwali.
Katika uwanja wa Stadium of Light, Sunderland walitoka sare tasa na Manchester United.
May 11, 2026 at 12:22PM
GAVANA Irungu Kang’ata wa Murang’a ameibuka tena kama mmoja wa viongozi wanaotikisa siasa za Mlima Kenya, baada ya kutangaza kuwa hatawania tena ugavana kwa tiketi ya UDA mwaka 2027, hatua iliyoibua mjadala mpana kuhusu mustakabali wake wa kisiasa.
Wadadisi wa siasa wanasema Kang’ata ni “twiga wa siasa” — kiongozi mwenye mtazamo wa mbali, na ambaye haogopi kusema ukweli hata ikiwa unaumiza maslahi ya walio mamlakani.
Kang’ata alithibitisha uamuzi wake wa kujiondoa kuwania tiketi ya UDA katika uchaguzi mkuu wa 2027, akisema alifikia uamuzi huo baada ya tafakari na mazungumzo ya ndani kushindwa kuleta muafaka.
“Mheshimiwa Rais amekuwa akituambia kila mara kwamba wananchi ndio wenye mamlaka ya mwisho. Nashukuru kwa kauli hiyo, na hivyo jukumu langu ni kufuata kile wananchi wamesema,” alitanguliza kwenye kikao na wanahabari Jumapili iliyopita.
“Kwa msingi huo, kwa kuwa nimejaribu kadri ya uwezo wangu kutatua masuala haya ndani ya chama, nimefanya mazungumzo ya wazi na Mheshimiwa Rais moja kwa moja, ambapo tulijadili mawazo haya lakini hatukufikia ‘muafaka kamili’,” akasema.
Hata hivyo, alisisitiza kuwa hana uhasama na Rais William Ruto au UDA akieleza kuwa ataendelea kuwa mwanachama mwaminifu hadi mwisho wa muhula wake.
“Hadi wakati huo nitasalia mwanachama mwenye nidhamu na aliyejitolea wa UDA. Nitaendelea kuhudumu kwa uaminifu katika wadhifa wangu na kushirikiana na serikali ya kitaifa,” akaeleza.
Kang’ata alifafanua zaidi msimamo wake wa kisiasa akisema halengi kiti kikubwa zaidi ya ugavana na kwa hivyo yeye si tisho kwa rais.
“Sina nia ya kugombea kuwa Rais wa Kenya wala sitaki kuwa Naibu Rais wa nchi. Kwa hivyo, maslahi yangu na yake hayagongani. Yangu ni kulinda kiti changu cha Murang’a pekee,” alisema.
Aliongeza kuwa bado hajachagua chama au jukwaa jipya atakalotumia mwaka 2027.
“Baada ya kutafakari kwa kina kuelekea 2027 sitatetea kiti changu kwa tiketi ya chama cha sasa. Baadaye nitatoa taarifa kuhusu jukwaa nitakalotumia kujitokeza mbele ya wapiga kura,” akaongeza.
Alidokeza kwamba amekuwa akishinikizwa kisiasa hasa wakati wa ziara za Rais katika kaunti yake.
“Nimeona kwa siku chache zilizopita, Rais amekuwa Murang’a, na kila ninapokwenda huko, ninashinikizwa kuunga mkono miradi yake,” alisema.
Kauli hizi zimezua athari za haraka ndani ya UDA, ambapo baadhi ya viongozi wa Murang’a wamemkosoa vikali.
Waziri wa Ardhi Alice Wahome na Mbunge Mary Wamaua walimshambulia gavana huyo wakisema ametema chama alichonufaika nacho kumpa kiti cha ugavana.
Lakini kwa wafuasi wake, Kang’ata ni kiongozi jasiri anayesema ukweli bila kuogopa mamlaka.
Historia yake ya kisiasa inaonyesha kwamba mara kadhaa amechukua misimamo migumu, ikiwemo kuonya hali ya Mlima Kenya kuelekea 2022 na sasa kutoa tahadhari kwa UDA kuhusu mwelekeo wake kuelekea 2027.
Katika mahojiano mengine wiki hii, Kang’ata alionyesha wasiwasi wake kuhusu mwelekeo wa siasa akisema: “Nimeona jinsi siasa zinavyoendelea, na sasa ninaamini kwamba hazitaishia vizuri kwa chama cha UDA, angalau katika eneo langu.”
Aliongeza: “Kinachonisikitisha ni kile UDA inachofanya kuhakikisha inabaki na uungwaji mkono. Nasema hivyo kwa sababu naamini kwamba kwa miaka miwili au mitatu iliyopita, kumekuwa na matendo ambayo yameimarisha upinzani.”
Kulingana na mdadisi wa siasa Dkt Isaac Gichuki, hatua ya Kang’ata sio ya kijasiri tu mbali ni ya mtu anayetazama mbali.
“Kang’ata amejisawiri kama kiongozi jasiri anayesema ukweli bila woga “twiga wa siasa” ambaye bado analenga mustakabali wa 2027 kwa macho ya mbali.
"Kilicho wazi ni kwamba Irungu Kang’ata ameendelea kujijenga kama mmoja wa viongozi wachache wanaoweza kusema “hapana” kwa mamlaka, na kubaki bado na ushawishi mkubwa wa kisiasa. Katika siasa za 2027, twiga huyu wa Murang’a bado anaonekana kuwa juu ya uwanja—akiona mbali kuliko wengine,” asema Dkt Gichuki.
May 11, 2026 at 08:40AM
WAZIRI wa Fedha, John Mbadi ameghairia nia kuhusu ahadi ya kupunguza ushuru wa mshahara kwa wafanyakazi walioajiriwa wanaolipwa chini ya Sh50,000.
Kwenye Mswada wa Fedha wa 2026, hakuna ushuru wa mapato ambao utapunguzwa, hili likiwa pigo kwa mamilioni ya waajiriwa ambao wanakumbwa na ugumu wa maisha baada ya mshahara wao kukatwa sana.
Serikali ilikuwa imeahidi kuondoa ushuru kwa Wakenya wanaolipwa mshahara wa hadi Sh30,000 kwa mwezi na kupunguza ushuru kwa mishahara ya chini ya Sh50,000.
Wafanyakazi hao wangepunguziwa kati ya Sh731 na Sh2,127.
Hazina iliachana na Mswada Spesheli wa Marekebisho ya Ushuru 2026 ambao ungesaidia katika utekelezaji wa makato hayo kwa wafanyakazi.
Mswada huo upo bungeni na unatarajiwa kupitishwa kufikia mwisho wa Juni.
“Tumeweka mswada huo kando kwa sababu tuna wiki chache tu kabla ya kuwasilishwa kwa Mswada wa Fedha 2026,” Bw Mbadi aliambia Kamati ya Bajeti bungeni Machi 31.
Badala yake Hazina Kuu imeongeza ushuru wa kodi ya nyumba, simu, pombe, sigara na kamari ili kupata Sh120 bilioni kwenye Mswada wa Fedha wa 2026.
Hii imepanda kutoka Sh30 bilioni ambazo serikali ililenga kwenye Bajeti ya 2025.
Hazina Kuu pia inalenga Sh81 bilioni kutoka kwa watu wasiolipa ushuru. Mamlaka ya KRA inatarajiwa kukusanya Sh2.985 trilioni kanzia Julai.
May 11, 2026 at 08:04AM
KUMEZUKA malalamiko mapya kufuatia uamuzi wa Rais William Ruto wa kufufua mpango wa malipo ya karo za shule kupitia mfumo wa e-Citizen, wakosoaji wakilaumu serikali kwa kupuuza hali halisi inayowakumba wazazi na shule nchini.
Wanaopinga mpango huo wamesema msimamo wa Rais wa kusisitiza utekelezaji wake unajiri licha ya upinzani kutoka kwa walimu wakuu, wazazi na mashirika ya elimu, pamoja na kesi inayoendelea katika Mahakama ya Rufaa kufuatia uamuzi wa Mahakama Kuu uliozima utekelezaji wa sera hiyo mwaka jana.
Akitetea agizo hilo Alhamisi, Rais Ruto alisema malipo ya kidijitali yataongeza uwazi na kupunguza mianya ya kupotea kwa fedha kwa njia ya pesa taslimu.
“Leo, mzazi anapaswa kulipa karo akiwa nyumbani kupitia e-Citizen, ambapo tunaweza kuthibitisha taarifa hizo. Nimeamua kimkakati kwamba, hatutaki tena kushughulika na fedha taslimu katika utawala huu kwa sababu pesa taslimu ni ngumu kufuatilia,” alisema katika mkutano wa pili wa elimu uliofanyika Naivasha.
Hata hivyo, wataalamu wa elimu na walimu wakuu wamesema hali halisi shuleni inafanya mpango huo kuwa mgumu kutekelezeka, kwa kuwa karo hulipwa kwa nyakati tofauti ilhali shule zinahitaji fedha za matumizi ya kila siku.
Mshauri wa sera katika shirika la Elimu Bora Working Group, Boaz Waruku, alisema shinikizo za serikali zinaonyesha kutojali changamoto za wananchi.
Alisema wazazi wa maeneo ya mashambani mara nyingi hulipa karo kwa njia mbadala kama kuni, chakula au kazi za mikono ili watoto wao waendelee kusoma licha ya ugumu wa kifedha.
“Mfumo wa e-Citizen unaweza kuwabana wazazi wanaolipa kwa njia ya mazao, kazi au makubaliano mengine na shule. Hali hii inaweza kuwafanya watoto kukosa elimu,” alisema.
May 11, 2026 at 07:55AM
TAHARUKI kuhusu uchaguzi imegubika jimbo la Louisiana kutokana na uamuzi uliotolewa wiki iliyopita na Mahakama ya Upeo uliobuni kipengee muhimu cha sheria kuhusu haki za umma.
Uamuzi huo uliwapa wabunge wa Republicans fursa ya kuchora ramani mpya inayofuta wilaya moja au mbili za Democratic katika jimbo hilo zenye idadi kubwa ya watu weusi.
Wapigakura wenye ngozi ya rangi nyeusi wanajumuisha thuluthi moja ya wapigakura jimboni Louisiana na kwa kawaida huunga mkono chama cha Democratic. Republicans tayari inadhibiti wilaya nyingine nne.
Siku moja baada ya uamuzi wa Korti ya Upeo, Gavana Jeff Landry aliahirisha chaguzi za vyama kuhusu ubunge nchini zilizopangiwa kufanyika Mei 16, hata ingawa maelfu ya madebe ya kura yalikuwa yamewasilishwa.
Wapigakura waliowasili sehemu za upigaji kura mapema wiki hii walikumbana na ilani zilizobandikwa kwenye milango zikitangaza kuwa chaguzi za ubunge zimefutiliwa mbali, huku vinyang’anyiro vingine vikiendelea.
Bado haijabainika kitakachofanyika kwa kura zilizokwisha kupigwa na ni lini chaguzi za vyama zitaratibiwa upya.
Maswali kuhusu mchakato huo yangesuluhishwa na katibu wa jimbo Louisiana, mwenyekiti wa kamati ya Republican, Caleb Kleinpeter alieleza wanahabari baada ya kusikizwa kwa kesi hiyo.
“Ukweli wa suala hili ni kuwa Mahakama ya Upeo ilikuja na ikasema ramani hizo ni kinyume cha katiba,” alisema. Kwa hivyo “tunasonga mbele na uchoraji wa ramani mpya”.
Akiwa mtoto, Leona Tate alikuwa moja kati ya wanafunzi weusi wa kwanza almaarufu “Wanne wa New Orleans” kujumuika katika shule ya umma mashinani Kusini, wakistahimili ubaguzi wa rangi na vitisho vya kuuawa, Jeshi la Nchi lilipowasindikiza darasani.
Ijumaa, zaidi ya miongo sita baadaye, Tate aliwaeleza wabunge wa Republican kwamba pendekezo lao la kuvunjilia mbali wilaya moja au zaidi zenye idadi kubwa ya watu weusi lilifufua kumbukumbu hizo za kutisha.
“Nataka mwelewe inavyohisi kusimama hapa, kutembea katikati ya halaiki ya watu kama mtoto, na sasa kuwatazama maafisa waliochaguliwa wakifanya jambo lile lile umma ulijaribu kufanya – tofauti tu ikiwa suti bora na mchakato wa bunge,” alieleza kikao cha kamati ya seneti katika jiji kuu la Baton Rouge.
Kwa zaidi ya saa nane, wabunge weusi wa Congress, mapasta, wanaharakati na wapigakura walitoa ushahidi ambao wakati mwingine ulivutia hisia za hasira na za kisiri.
Nje ya chumba cha kusikiza kesi, umati uliwashangilia kuendelea.
“Acha azungumze!” Waliimba wakati mmoja baada ya Kleinpeter kuzima kipaaza sauti cha mbunge mwenzake wa Democratic katikati ya majibizano makali.
Mike McClanahan, rais wa shirika kubwa zaidi la kutetea haki za kibinadamu nchini kwa jina NAACP, Louisiana, alizuiwa kimabavu kuingia chumba hicho na ulinzi wa seneti.
Louisiana ndiyo ya hivi majuzi kwenye mzozo kitaifa unaohusu mchakato wa kuunda upya wilaya ulioanzia Texas mwaka jana na kushika kasi wiki hii kote Kusini ikiwemo Tennessee, Alabama na South Carolina, ambapo wana Republicans walijibu maamuzi ya korti ya upeo kwa kuanzisha juhudi sawia za kuangamiza wilaya zinazosheheni idadi kubwa ya weusi.
Wanademocrats wameanzisha juhudi zao binafsi za kuunda upya wilaya, lakini azma yao ilipata pigo kuu Ijumaa wakati Mahakama ya Upeo Virginia ilipotupilia mbali ramani mpya iliyopitishwa na wapigakura ambayo huenda ingebadilisha viti vinne vya Republican.
Kilichokuwa kinyang’anyiro chenye usawa cha kuchora upya ramani za bunge sasa kimegeuka kwa kishindo kuegemea Republican kabla ya uchaguzi wa katikati ya muhula November, ambapo itatetea idadi iliyobanwa ya waliowengi bungeni.