Taifa Leo | Kenya Live News
Sat
27
Jul
24
Jul 27, 2024 at 08:55AM
UMAARUFU wa mgombea urais wa chama cha Democratic Kamala Harris unatarajiwa kupanda hata zaidi baada ya kupata uungwaji mkono kutoka kwa Rais wa zamani Barack Obama na mkewe, Michelle. Kwenye video iliyoonekana kunaswa wakati wa shughuli za kampeni, Makamu wa Rais anajibu simu kutoka kwa Obama kupitia simu yake ya mkononi. “Nakupigia kukuarifu kwamba ni fahari yangu na Michelle kukuunga mkono na tutafanya kila tuwezalo kukuwezesha kushinda uchaguzi huu na kuingia Ikulu,” Rais huyo wa zamani anasikika akisema. Makamu wa rais huyo wa Amerika Alhamisi alisaka uungwaji mkono katika shirikisho kubwa zaidi la walimu nchini humo huku matokeo ya kura ya maoni yakionyesha anamkaribia rais wa zamani Donald Trump. Kuibuka kwa Harris kama mgombea urais wa chama tawala cha Democrat baada ya kujiondoa kwa Rais Joe Biden, 81, kumeleta msisimko mpya katika kinyang’anyiro cha urais nchini Amerika. Makamu huyo wa Rais anatarajiwa kuidhinishwa rasmi kuwa mgombea urais wa chama cha Democratic katika Kongamano la Kitaifa la chama hicho jijini Chicago, jimbo la Illinois mwezi ujao. Harris atapambana na Trump wa chama kikuu cha upinzani Republican katika uchaguzi wa urais mnamo Novemba 5, mwaka huu. Akihutubu jijini Houston katika Kongamano la Shirikisho la Walimu Amerika (FAT), Harris, 59, aliangazia zaidi sera za kiuchumi na haki za wafanyakazi. Aliahidi kuendeleza mipango ya utoaji huduma nafuu za afya na utunzaji watoto. Aidha, Harris aliwakashifu vikali viongozi wa chama cha Republican kwa kupinga utekelezaji wa sera ya kudhibiti umiliki wa bunduki kama njia ya kukomesha visa vya mashambulio ya risasi shuleni. “Tunaongozwa na haja ya kupigania maisha mazuri siku zijazo,” Harris akauambia umati wa karibu watu 3,500. “Tuko katika mapambano ya kupigania na kulinda haki za kimsingi na uhuru; haki za walimu wetu na watoto wetu,” akaongeza. Baadaye zaidi ya wanawake 100,000 wa asili ya Waamerika weupe waliungana katika mtandao wa Zoom kuchanga pesa za kufadhili kampeni za Harris kando na kujadili mikakati ya kuendesha kampeni hizo. Mchango huo unafuatia mwingine ulioendeshwa siku chache zilizopita na wanawake Weusi, wanaume Weusi na watu wa asili ya Latino. Kura kadhaa za maoni zilizoendeshwa tangu Biden alipojiondoa katika kinyang’anyiro cha urais Jumapili iliyopita, ikiwemo kura ya Reuter/Ipsos, zinaonyesha kuwa Harris na Trump wanaanza kukaribiana kwa umaarufu. Hii inaashiria kuwa wawili hao wataendesha kampeni kali zaidi katika muda wa miezi mitano na nusu ijayo. Matokeo ya kura ya maoni yaliyoendeshwa na gazeti la New York Times na chuo cha Siena College na kuchapishwa Alhamisi yalionyesha Harris akimkaribia Trump, japo mgombeaji huyo wa Republican bado akiongoza. Trump alikuwa mbele ya Harris kwa kuandikisha umaarufu wa asilimia 48 dhidi ya asilimia 46, miongoni mwa wapigakura waliosajiliwa. Mapema mwezi huu wa Julai Trump alikuwa na umaarufu wa asilimia 49 mbele ya Biden aliyekuwa na umaarufu wa asilimia 41. Hii ni baada ya Biden kufanya vibaya zaidi katika mdahalo kwa kwanza wa urais kati yake na Trump. Ni kufuatia mdahalo huo ulioendeshwa na shirika la habari la CNN ambapo wafuasi wa chama cha Democrat walianza kumwekea Biden presha ajiondoe kinyang’anyironi. Aidha, Harris alipata habari katika kura ya maoni katika majimbo matano muhimu nchini Amerika. Kulingana na matokeo ya kura ya maoni yaliyochapishwa na Emerson College/The Hill, Makamu huyo wa Rais alianza kumkaribia Trump, kwa umaarufu katika majimbo kama vile: Arizona, Georgia, Michigan, Pennsylvania na Wisconsin.
Jul 27, 2024 at 07:55AM
POLISI mjini Kisii wanachunguza kisa ambapo Wakristo kumi wa Kanisa la Kiadventista (SDA) la Nyabigena wanasemekana kujeruhiwa baada ya mapigano kuzuka kanisani humo Jumamosi iliyopita wakati wa ibada. Chanzo cha machafuko hayo kinasemekana kusababishwa na mzozo unaohusisha makongamano mawili yanayong'ang'ania umiliki wa kanisa hilo. Kulingana na Bi Martha Bosibori-mmoja wa waathiriwa- mzozo kati ya makongamano hayo umekuwepo kwa muda sasa. Kila kongamano linadai kumiliki kanisa hilo. "Kulizuka fujo wakati mmoja wa wazee wa kanisa alipotangaza kwa waumini wengine kwamba kulikuwa na wasaliti waliokuwa wamehudhuria ibada ya Sabato iliyopita. Mara tu alipomaliza kutoa tangazo hilo, watu wasiojulikana walivamia kanisa na kuanza kuwavuruga waumini na kizaazaa kilishuhudiwa," Bi Bosibori alidai. Katika video inayoonyesha matukio yaliyojiri ndani ya majengo ya kanisa hilo, waliohusika katika machafuko hayo wanaonekana wakishambuliana kwa mateke na ngumi. Viti vya plastiki vinatupwa kote huku wale wanaopigana wakijaribu kulimana visawasawa. Wanawake wanasikika wakipiga nduru kwa kustaajabishia kile kilichowapata. "Hili ni kanisa la aina gani sasa? Mbona unanipiga ninapojaribu kuwaokoa baadhi ya watu wetu?" Sauti ya mwanamke inasikika ikiuliza kwenye video hiyo. Kufikia kuandikwa kwa taarifa hii, uongozi wa kanisa la SDA bado haukuwa umetoa taarifa yoyote kuhusu suala hilo. [caption id="attachment_156157" align="alignnone" width="300"] Kanisa la Kiadventista (SDA) la Nyabigena. Picha| Hisani[/caption] Taifa Leo ilipowasili kanisani humo, ilikutana na kundi la wazee na wachungaji wakiwa wamejikita katika mkutano. "Hebu kwanza tushauriane na tuone kama tutawahutubia," mmoja wa washiriki wa mkutano huo alisema bila kujitambulisha. Licha ya kufanya wanahabari wetu kusubiri nje ya kanisa hilo kwa zaidi ya masaa matatu, kundi hilo mwishowe halikufanya kweli kuhusu ahadi yao kwani halikutoa taarifa yoyote. Badala yake wazee hao walisema tuje kuangazia maandamano ambayo walisema walikuwa wakiyapanga. Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Nyamarambe Thomas Parkolwa, alithibitisha kutokea kwa hitilafu hizo na kusema wameanzisha uchunguzi wao. "Tuliitwa huko baada ya mzozo kutokea. Si kazi yetu kuamua nani anamiliki kanisa lakini watu wanapokuwa na vurugu, tunapaswa kuwajibika. Maafisa wetu wamelishughulikia suala hilo na tumeanza uchunguzi. Tulipofika kanisani, hakuna mtu aliyekuwepo na walikuja kuripoti tu wakati mapigano hayo yalikuwa yameisha," Bw Parkolwa aliambia Taifa Leo kwa simu. Mkuu huyo wa polisi alikashifu kundi moja ambalo alisema halikuwa tayari kushirikiana nao. “Tumejaribu kuwapatanisha, tumewaomba waangazie njia nyingine za kutatua mgogoro uliopo lakini kuna kundi ambalo halitaki kusikia chochote, wao ndio waliotoa video ya mapigano wakitaka isambae mitandaoni. Inasikitisha sana kwamba matukio kama haya yanaweza kutokea katika kanisa la kisasa," kamanda huyo aliongeza. Aliwataka wakaazi au mashirika mengine yoyote kutafuta njia zingine za kutatua migogoro badala ya kupigana.
Jul 27, 2024 at 06:55AM
MCHESHI David Oyando almaarufu Mulamwah, amewataka mashabiki wa mitandao ya kijamii, kuunga 'babymama' wake Caroline Muthoni almaarufu Carol Sonnie, pamoja na mke wake Ruth K, kwa kazi wanayofanya mitandaoni ili kujipatia riziki ya kujiendeleza kimaisha. Katika mahojiano, mcheshi huyo aliwataka mashabiki wao kukoma kurusha vijembe vya matusi ambavyo alieleza huwatatiza wawili hao. “Mtandaoni kuna mambo mengi yanaendelea, kuna timu upande huu na ule. Matusi ni ya nini?” aliuliza Mulamwah. “Nataka, hawa wanawake wawili wajijenge kwa kupata riziki kupitia hiyo mitandao. Naomba mashabiki wawasaidie ili kila mmoja wao akue kimapato. Haina haja nyinyi mwendeleze matusi kwao. Adui wa mwanamke asikuwe mwanamke tena,” aliongeza Mulamwah. Aliongeza kuwa baadhi ya matusi hayo hufanya wazazi wao kupatwa na huzuni. “Unaporusha cheche za matusi kwa hawa wanawake wawili, kumbuka sio wao tu wanapatwa na matatizo ya kiakili, bali pia wazazi wetu wanahuzunika,” alieleza. Mulamwah,31, alisema wito wake wa kutaka warembo hao kukosa kudhalilishwa mitandaoni ni baada ya mzazi mwenza (Carol Sonnie) baada kutoa habari kuwa hana chuki naye. “Kila wakati nimekuwa nikilaumiwa mimi ndiye humkosea kila ninaposema pale mitandaoni. Juzi kwenye mahojiano fulani alisema hana chuki nami na ndio maana nasema tuache chuki na uhasama,” aliongeza. Baba huyo wa watato watatu alisema kuwa tayari ana amini kukutana na aliyekuwa mpenziwe wa zamani kuhakikishia ulimwengu wako sawa. “Hii wiki lazima tutakutana na Sonnie ili mjue tuko sawa. Na kama hatutakutana mjue kuwa mambo si sawa.” Mulamwah ambaye siku za hivi karibuni alifanya sherehe ya kufichua sura ya mwanawe wa kiume na kufichua kuwa kifungua mimba wake ana umri wa miaka mitatu, alieleza sababu ya kukosa kujieleza kwa nini waliachana na 'babymama' Carol Sonnie. “Wengi hamjui kuwa tulitengana naye alipokuwa mjamzito na miezi saba au nane. Nilimuahidi nitajukumika lakini tukawa tumejadiliana ni wakati upi tutafahamisha ulimwengu. Miezi sita baadaye akasambaza mitandoni. Kila mmoja akanichukia na kunichukulia mbaya.”  “Nilianza kukasirika, nikaanza kujibu kwa kuchapisha vitu ambavyo havikuwa vinafaa. Ninaamini Mungu alinishikilia, ikawa sikuposti kila kitu kwani vikisemwa, vitaathiri vibaya maisha ya watu wengine na kuchukuliwa vibaya,” alisema Mulamwah. Mulamwa alibainisha kuwa matukio yaliyofuata baada yaa chapisho lake, hayajakuwa mazuri kwani yeye na Carol walipitia unyanyasaji mwingi kwenye mitandao ya kijamii kuhusu mtoto wao.
Jul 27, 2024 at 05:55AM
JUHUDI za kiongozi wa ODM Raila Odinga za kuokoa serikali ya Rais William Ruto aliye katika shinikizo lililosababishwa na maandamano ya vijana, zimefufua mjadala kuhusu mtindo wake wa kusaliti washirika wake wa kisiasa. Japo si mara yake ya kwanza kuingia katika ukuruba wa kisiasa na serikali baada ya kushindwa katika uchaguzi, ni mbinu yake ya kufanya hivyo inayozua mdahalo hasa wakati huu ambao vijana wanashinikiza utawala bora. Huku wanaounga serikali wakimtaja kama mzalendo kwa kuokoa nchi wakati wa mizozo mikubwa ya kisiasa, washirika wake wanamuona kama msaliti. Baada ya wandani wake kuteuliwa mawaziri katika serikali ya Kenya Kwanza ambayo awali alikuwa akiikosoa vikali kwa kubebesha raia zigo la gharama ya maisha, vinara wenza katika muungano wa upinzani wa Azimio la Umoja One Kenya wamemtaja kama msaliti kwa kuwa walikuwa wameapa kutojiunga na serikali. Tukio la Jumatano, Rais William Ruto alipowateua washirika wanne wa karibu wa Raila kwenye baraza jipya la mawaziri, lilizidisha mvutano hata ndani ya ODM na Azimio, huku kiongozi wa chama cha Narc Kenya, Martha Karua akiwasilisha notisi ya kujiondoa katika muungano huo. Kuna ripoti kwamba hatua ya Raila ilinuia kuvunja muungano huo japo anasisitiza wandani wake John Mbadi, Wycliffe Oparanya, Hassan Joho na Opiyo Wandayi waliteuliwa kama watu binafsi na sio kwa uamuzi wa chama. Kauli za wabunge wa ODM zinaonyesha kuwa ulikuwa uamuzi wa chama hicho cha Chungwa. “Ninataka nimpongeze Rais kwa uteuzi huo lakini pia ninaomba ndani ya wiki moja, mara tu kesho, tuone majina ya wateule ambao Baba alipeleka leo na tunataka wote wapitishwe, na ikiwezekana basi, hii ifanyike haraka sana. Kama chama cha ODM, tulikaa na kusema serikali ya Kenya ni yetu sote. Tulikutana na kuamua,” mbunge wa Homa Bay Mjini Peter Kaluma alisema Jumanne kabla ya Rais kutangaza majina ya wanachama wa ODM kuwa mawaziri Jumatano. Karua aliyekuwa mgombea-mwenza wa Raila katika uchaguzi mkuu wa 2022 ambao Rais William Ruto na naibu wake Rigathi Gachagua waliibuka washindi, alisema matukio ya kisiasa nchini yanafanya Narc Kenya kutoendelea kuwa katika Azimio la Umoja. Baada ya uchaguzi mkuu wa 2018, Bw Odinga aliwaacha washirika wake katika uliokuwa muungano wa Nasa na kuanza ukuruba wa kisiasa na Rais Uhuru Kenyatta ambaye wadadisi wa siasa wanasema alikuwa mateka wa naibu wake Dkt Ruto. Hatua yake iliyozaa uhusiano wa kisiasa uliofahamika kama handisheki ilifanya Nasa kusambaratika na kumrahisishia Uhuru muhula wake wa pili, Dkt Ruto akitengwa katika serikali ya Jubilee. Inasemekana kuwa chini ya ukuruba wake wa kisiasa na Bw Uhuru, alikataa washirika wake kuteuliwa serikalini, jambo ambalo amekubali chini ya usuhuba wake na Rais Ruto. Akizungumza katika mkutano wa Baraza Kuu la kitaifa la ODM na kundi la wabunge kabla ya wandani wake kuteuliwa mawaziri, Raila alionekana kuunga mkono utawala wa Dkt Ruto akikosoa presha za vijana kutaka Rais ajiuzulu, akisema shinikizo hizo zina athari hasi. "Ruto aende, basi nini? Ruto huenda akaondoka, kisha Rigathi Gachagua achukue hatamu, bado atatekeleza sera mbovu. Ruto pia anaweza kusema nimechoka, acha majenerali (wanajeshi) wachukue madaraka. Ruto lazima aende, haiwezi kuwa suluhu,” Bw Odinga alinukuliwa akisema siku chache kabla ya Rais kuwateua wandani wake. "Ni wakati wa shida kama huu ambapo nchi inahitaji kuzungumza. Hatufanyi hivyo ili kumwokoa Ruto. Tunafanya hivyo kuokoa Kenya,” aliongeza. Kulingana na wadadisi wa siasa, Raila amemuokoa Ruto aliyeonekana kuwa mateka wa naibu wake Bw Gachagua ambaye alikuwa ametangaza serikali ya Kenya Kwanza kuwa ya hisa za jamii na maeneo yaliyoipigia kura kwa wingi. “Raila Odinga hatabiriki sana kwa sababu unapofikiri kwamba yuko nje, anaibuka tena na mara nyingi, huwapata marafiki zake wa karibu kwa mshangao,” alisema Prof Masibo Lumala wa Chuo Kikuu cha Moi katika mahojiano ya awali. Kinyume na ilivyokuwa alipomuokoa Bw Uhuru 2018, ukuruba wake na serikali ya Rais Ruto umezua minong’ono katika chama chake, baadhi ya wabunge wake wakieleza kukerwa na uamuzi wa viongozi wao wanne kujiunga na serikali na kupuuza matakwa ya vijana. “Kwa kuokoa Ruto, sawa na alivyofanya alipomuokoa Uhuru, Raila amesaliti tena washirika wake wa kisiasa na kwa kiwango kikubwa vijana ambao malalamishi yao kwa serikali ni ya kweli. Wanasiasa wenzake wanaweza kumsamehe kwa kuwa hakuna uhasama wa kudumu katika siasa, lakini vijana hawataweza ikizingatiwa ametumia shinikizo zao kwa manufaa ya kibinafsi kujiunga na serikali kupitia washirika wake,” asema Prof Isaac Gichuki. Wadadisi wanasema Bw Raila pia amemsaliti Uhuru aliyeokoa jahazi lake la kisiasa kabla ya uchaguzi wa 2022 kwa kuunda Azimio, muungano wa Nasa ulipovunjika kufuatia madai Bw Raila aliwasaliti waliokuwa washirika wake wakiwemo Musalia Mudavadi, Kalonzo Musyoka na Moses Wetang’ula.
Jul 26, 2024 at 06:55PM
MKAZI mmoja wa hapa amechanganyikiwa baada ya kugundua kuwa mkewe aliyemsamehe kwa kuchepuka, alikuwa na mimba ambayo anashuku sio yake. Jombi alimfumania mkewe akitoka gesti na buda mmoja na mwanadada akakiri alikuwa akishiriki mpango wa kando na mwanamume huyo na akaahidi kuacha. Jamaa alimsamehe lakini baada ya wiki tatu akagundua demu alikuwa na mimba. Kwa kuwa alikuwa akichepuka na ufichuzi huo ulijiri muda mfupi baada ya kumsamehe demu, jamaa alichanganyikiwa asijue la kufanya hadi akaanza kulewa kupindukia. Juzi, alifunguka na kumweleza kaka yake kinachomsumbua na akashauriwa amuulize mkewe mimba ilikuwa ya nani. Lakini alipomuuliza mkewe alichanganyikiwa zaidi alipomuuliza iwapo hakuwa amemsamehe kwa dhati.
Jul 26, 2024 at 06:28PM
MWANAHARAKATI Boniface Mwangi na wengine wanne waliokamatwa Alhamisi wakiandamana dhidi ya serikali wameachiliwa kwa dhamana ya pesa taslimu Sh20,000 kila mmoja. Akiwaachilia huru, Hakimu Mkuu wa Milimani Gilbert Shikwe alimuonya Bw Mwangi na wenzake wanne kutoingilia uchunguzi. Akikataa ombi la polisi la kuwazuilia Mwangi, Robert Otieno, Albert Wambugu, Pablo Chacha na Erot Franco kwa siku 21 hakimu huyo alisema makosa yanayochunguzwa ni madogo. Shikwe alisema polisi wanaweza kuchunguza makosa, washukiwa wakiwa nje kwa dhamana. Aliwaagiza washukiwa hao kushirikiana na wapelelezi kabla ya kuagiza kesi hiyo itajwe Agosti 16 2024 kwa maagizo zaidi. Hakimu alikubaliana na mawakili wa utetezi kwamba dhamana ni haki ya kikatiba. "Dhamana ni haki ya kikatiba kwa washukiwa ambao wako chini ya uchunguzi wa polisi," Shikwe aliamua. Pia alisema hakuna sababu za msingi za kuitaka mahakama kuwanyima dhamana washukiwa hao.
Jul 26, 2024 at 05:34PM
UTEUZI wa viongozi wakuu wa chama cha upinzani ODM kwa nyadhifa za uwaziri sasa unaning'inia hewani kufuatia mwanaharakati mmoja kukimbilia mahakamani kupinga zoezi hilo. [caption id="attachment_156142" align="alignnone" width="300"] Mwanaharakati Julius Ogogoh ambaye amefikisha kesi kortini. Picha|Maktaba[/caption] Mwanaharakati Julius Ogogoh amefikisha ombi kortini Ijumaa akitaka uteuzi wa Hassan Joho (kwa Wizara ya Madini na Uchumi wa Baharini), John Mbadi (Wizara ya Fedha), Wycliffe Oparanya (Wizara ya Vyama vya Ushirika) na Opiyo Wandayi (Wizara ya Kawi) uvunjiliwe mbali, akidai kwamba haukufuata katiba. Bw Ogogoh, kupitia Tume ya Kutetea Haki za Kibinadamu, amewasilisha kesi katika Mahakama Kuu akiitaka izuie Bunge la Kitaifa kuwapiga msasa Joho, Oparanya, Mbadi na Wandayi ili wateuliwe rasmi kuhudumu kama mawaziri. Bw Ogogoh anasema Kenya inazingatia demokrasia ya vyama vingi na mbunge hawezi kujiunga na chama kingine baada ya uchaguzi. Aidha, anasema kuwa uteuzi wa wanne hao utadhoofisha upinzani ndani ya bunge na kuhujumu utendakazi wa bunge kama asasi ya kuhakiki utendakazi wa serikali kuu. “Endapo mwanachama wa mshtakiwa wa kwanza (Azimio) atateuliwa kuwa waziri upinzani ndani ya bunge utadhoofishwa hali ambayo ni kinyume cha Kipengele cha 75 cha Katiba,” akasema. Mabw Oparanya na Joho ni manaibu wa Bw Raila Odinga ambaye ni kiongozi wa ODM ilhali Bw Mbadi ni mwenyekiti wa chama hicho. Naye Bw Wandayi, ambaye ni Mbunge wa Ugunja, ni Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa na Katibu wa Masuala ya Kisiasa katika ODM. Majina yao yamewasilishwa kwa Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula ambaye ameweka tangazo magazetini akiomba umma kuwasilisha memoranda kuhusu ufaafu wa mawaziri hao wateule. Lakini Bw Ogogoh anataka mahakama kuu ibatilishe uteuzi wa wanne kwa misingi kuwa umefanywa kinyume cha katiba. Ameorodhesha muungano wa Azimio la Umoja-One Kenya, chama cha ODM, Bw Wetang’ula na Mwanasheria Mkuu kama washtakiwa katika kesi hiyo. Kupitia wakili, Nicholas Kamwenda, Bw Ogogoh anasema wanne hao ni wanachama wa Azimio na hivyo hawawezi kuteuliwa kuhudumu kama mawaziri. “Kwa kuwa upinzani katika Bunge la Kitaifa una wajibu wa kikatiba wa kuhakikisha utendakazi wa Serikali Kuu na matawi mengine ya serikali, hautaweza kutekeleza wajibu huo ipasavyo ikiwa wabunge wa mrengo huo watateuliwa kuwa mawaziri,” akasema. Bw Ogogoh anaeleza kuwa hatua hiyo inaenda kinyume na wajibu ambao Wakenya wanataraji utekelezwe na upinzani. “Matokeo ya uteuzi wa wabunge wa upinzani kujiunga na serikali ni kwamba hakutakuwa na upinzani katika Bunge la Kitaifa. Hakutakuwa uhakikisha wa serikali na matawi mengine na hivyo hayatawajibika kwa raia wa Kenya wanaopasa kuhudumiwa,” akasema. Kulingana na Ogogoh hatimaye maovu yataendelea serikalini na maafisa wake hawawajibika ipasavyo.
Jul 26, 2024 at 02:40PM
SIKU chache baada ya Rais William Ruto kumteua aliyekuwa Gavana wa Mombasa Bw Hassan Ali Joho kama Waziri wa Madini na Uchumi wa Baharini, wakazi wa Taita Taveta sasa wana matumaini kuwa watanufaika kutokana na madini yaliyoko katika eneo hilo. Kaunti ya Taita Taveta imejaaliwa na madini mengi yakiwemo vito vyenye thamani haswa Tsavorite, inayopatikana mbugani Tsavo pekee. Hata hivyo, kwa miaka mingi, wachimbaji wamekuwa wakilalamikia kutonufaika kutokana na madini hayo na hivyo kutoona manufaa ya uchimbaji wao. Iwapo ataidhinishwa na bunge, Bw Joho atarithi mipangilio mingi ya sekta hiyo katika kaunti hiyo iliyokuwa imewekwa na mtangulizi wake Bw Salim Mvurya, ikiwemo kujengwa kwa kiwanda cha chuma, wachimbaji kuruhusiwa kuchimba mbugani Tsavo, utoaji wa leseni haswa kwa wachimbaji wadogo wadogo miongoni mwa mengine. Baadhi ya wachimbaji wa eneo hilo waliambia Taifa Leo kuwa wana matumaini kuwa Bw Joho ataweza kusukuma mbele sekta hiyo kwa manufaa ya wenyeji. Akiongea mjini Mwatate, mwenyekiti wa wachimbaji wadogo katika kaunti hiyo Bw David Zowe, alitaja kuwa vito vya Tsavorite vimetajwa kuwa miongoni mwa madini ya kimkakati. Alimtaka Bw Joho kuunga mkono kuondolewa kwa jiwe hilo katika orodha ya madini hayo. "Ninashukuru Rais kwa kumteua Bw Joho na tunamuomba punde tu atakapochukua hatamu ya afisini, ashughulikie changamoto zinazotukumba sisi wachimbaji wadogo zikiwemo kuondolewa kwa Tsavorite miongoni mwa orodha ya madini ya kimkakati," akasema. Alisema kuwa leseni ambazo serikali inawapa wachimbaji na wauzaji wa madini kwa sasa, zimewanyima nafasi ya kuchimba na kuuza Tsavorite. "Tunakuomba kwanza uunde mikakati na kuwasilisha ombi kwa baraza la mawaziri kukubalia uchimbaji na uuzaji wa Tsavorite," akasema. Vilevile, alisema kuwa wanatarajia Bw Joho kuidhinisha kamati ya kusimamia shughuli za jengo la vito lililoko mjini Voi ili liweze kutoa huduma kwa wananchi jinsi inavyopaswa. "Tunatarajia ahakikishe wachimbaji wadogo wanapata maeneo ya kuchimba madini nje na ndani ya mbuga ya Tsavo. Bado serikali haijatupa maeneo ya uchimbaji," akasema. Mchimbaji mwingine Bi Mariam Chirera, alisema kuwa renchi za eneo hilo vilevile zitanufaika kutokana na shughuli za uchimbaji katika maeneo hayo. "Mimi ni mwanachama wa renchi ya Wushumbu na tunategemea sana uchimbaji wa vito. Tunajua kuwa Bw Joho ni mchapakazi na atatusaidia kuendeleza shughuli hizo katika renchi zote 31 za hii kaunti," akasema. Kaunti hiyo pia imejaliwa na uwepo wa madini ya chuma katika eneo la Kishushe. Kwa sasa, serikali inapangilia kuanzishwa kwa mtambo wa chuma unaotarajiwa kujengwa katika eneo la Ngolia na kampuni ya Devki Steel Mills. Mtambo huo utakaogharimu Sh11 bilioni, unatarajiwa kubuni nafasi za kazi kwa mamia ya wakazi na vilevile kuboresha uchumi wa eneo hilo. Hata hivyo, uchimbaji wa madini ya chuma katika renchi ya Kishushe umekumbwa na mizozo baina ya mwekezaji, wenye renchi na wananchi. Kwa sasa, mwekezaji huyo, Samruddha Resources Kenya Limited, amesimamisha shughuli zake baada ya renchi ya kishushe kuwanyima kibali cha uchimbaji. Wananchi na viongozi wa eneo hilo wamekosa imani na mwekezaji huyo kwa kutowajibika kufanya miradi ya kijamii kama inavyotakikana kisheria. Tangu mnamo Machi mwaka jana, mwekezaji huyo alitakiwa kulipa Sh30 milioni za miradi ya kijamii lakini hadi leo, amelipa Sh25 milioni pekee. Aidha, wenyeji wa Kishushe wamekataa kamati iliyokuwa imeteuliwa na aliyekuwa waziri Bw Mvurya kusimamia miradi itakayotekelezwa kupitia fedha hizo.
Jul 26, 2024 at 01:40PM
RAIS William Ruto ametetea hatua yake ya kujumuisha viongozi wa upinzani katika serikali yake akisema kuwa ananuiwa kuhakikisha kuwa Wakenya wote wanashiriki katika ujenzi wa taifa. Rais alisema ili kutatua changamoto zinazokabili taifa kutokana na maandamano ya Gen Z na wanaharakati, alifanya uamuzi mgumu wa kujumuisha upinzani katika utawala wake. Maandamano hayo yalimfanya rais kuondoa Mswada wa Fedha wa 2024 ambao ulikuwa umependekeza Wakenya kutozwa ushuru mkubwa na kufuta baraza lake lote la mawaziri. Siku ya Jumatano, Rais aliwateua wanasiasa wa upinzani katika baraza lake la mawaziri ambao watapigwa msasa na bunge. Wanajumuisha mwenyekiti wa ODM John Mbadi (Hazina na Mipango ya Kitaifa) Wycliffe Oparanya (Biashara na Vyama vya Ushirika), Hassan Joho (Madini na Uchumi wa Baharini) na Opiyo Wandayi (Kawi na Petroli). Dkt Ruto alikariri kuwa hatua yake itaunganisha taifa kwa manufaa ya Wakenya wote na kuipeleka nchi katika viwango vya juu vya maendeleo. “Nimeamua tuunde serikali ambayo itatuunganisha sote ili kila Mkenya sasa ashiriki katika ujenzi wa taifa. Kuanzia sasa na kuendelea, sote tutatafuta njia za kuongeza mapato pamoja na kulipa madeni yetu. Hakuna atakayeachwa nyuma,” alisema. Rais alizungumza Alhamisi katika mji wa Marimanti katika Kaunti ya Tharaka Nithi ambapo alizindua miradi ikijumuisha mradi wa maji wa Sh180 milioni katika eneo bunge la Kibung’a. Pia alizindua jengo la ofisi la kamishna wa kaunti na kituo cha Huduma. Aliandamana na naibu wake Rigathi Gachagua, aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Prof Kithure Kindiki ambaye ameteuliwa kuhudumu katika wadhifa huo na Gavana wa Tharaka Nithi Muthomi Njuki. Wengine walikuwa Naibu Spika wa Seneti Kathuri Murungi, Mwenda Gataya (Seneta Tharaka Nithi) mwakilishi wa wanawake wa Meru Elizabeth Kailemia na mwenzake wa Tharaka Nithi Susan Muindu, wabunge Gitonga Murugara (Tharaka), Mpuru Aburi (Tigania Mashariki) Patrick Munene (Igambang'ombe) na Kareke Mbiuki (Maara). Dkt Ruto alimmiminia Prof Kindiki sifa na kumtaja kuwa mmoja wa mawaziri waliofanya kazi kwa bidii katika utawala wake, akisema hiyo ndiyo sababu aliyomteua kuhudumu katika baraza lake jipya la mawaziri. “Prof Kindiki aliangamiza ujangili katika kaunti na alifanya kazi nzuri. Kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi hii baadhi ya shule huko Baringo zilifunguliwa tena baada ya zaidi ya miaka 15. Pia alikabiliana na magaidi na kuhakikisha kuwa nchi yetu iko salama. Mtu akifanya kazi nzuri ni lazima apongezwe,” rais alisema. Dkt Ruto aliahidi kuwa serikali yake itahakikisha miradi ya maendeleo inatekelezwa nchini na kuahidi ujenzi wa nyumba 500 katika makao makuu ya kaunti ya Tharaka Nithi mjini Kathwana.
Jul 26, 2024 at 10:55AM
KIONGOZI wa Upinzani Raila Odinga jana alikanusha kuwa ana mkataba wa kisiasa na UDA inayoongozwa na Rais William Ruto licha ya maafisa wake wanne kuteuliwa mawaziri mnamo Jumatano. Katika hatua iliyoonekana kujaribu kuepuka hasira za vijana wanaomlaumu kwa hatua ya kukubali kuungana na serikali wanayopinga, Bw Odinga alisema chama na Azimio hazikuamua kushirikiana na Kenya Kwanza. Bw Odinga kupitia taarifa jana alisema wanne hao John Mbadi, Hassan Joho, Opiyo Wandayi na Wycliffe Oparanya, wamejiunga na utawala wa Kenya Kwanza kama watu binafsi. Hata hivyo, hakubainisha iwapo aliwapa baraka zake huku akiwatakia kila la kheri na kuwataka watumie vyeo hivyo kubadilisha nchi. “Jinsi ilivyoandikwa kwenye taarifa yetu mnamo Julai 23, 2024 ODM au Azimio la Umoja hazijaungana na utawala wa Rais William Ruto,” akasema Bw Odinga. Aliongeza kuwa, ODM ilikuwa inatarajia kushirikiana tu na serikali baada ya kuundwa kwa mwongozo wa kuyatatua masuala ambayo yaliibuliwa na Gen Z. Kati ya masuala hayo ni fidia kwa familia ambazo watu wao waliuawa baada ya kutekwa, wale waliojeruhiwa wakati wa maandamano ya upinzani mwaka jana na kushtakiwa kwa polisi ambao waliwaua waandamanaji. “Japo tunawatakia walioteuliwa kila la heri na kuonyesha imani watachangia kujenga taifa hili, bado tunapigia debe mazungumzo kwa msingi wa masharti ambayo tuliyatoa,” akasema. Kauli hii ilionekana kurejelea matakwa ya vijana na vinara wenza wa Azimio ambao wamekataa kujiunga na serikali. Bw Odinga alisema chama chake kinasalia imara katika kudumisha msingi wa demokrasia, uongozi bora na haki ya kijamii. Hata hivyo, hatua ya ODM kusisitiza kuwa haijajiunga na UDA inaonekana kama mbinu ya kuhakikisha inasalia na viti viwili vya hadhi katika uongozi wa bunge. Iwapo ODM ingekubali kuwa imeanza ushirikiano wa kisiasa na Kenya Kwanza, basi vyama tanzu ndani ya Azimio hasa Wiper na Jubilee ya Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta, vingeendea nyadhifa za Kiongozi wa Wachache na Uenyekiti wa Kamati ya Uhasibu Bungeni (PAC). Nyadhifa hizo mbili zilikuwa zikishikiliwa na Wandayi na Bw Mbadi ambao hawatakuwa na jingine ila kujiuzulu iwapo uteuzi wao wa kuunga baraza la mawaziri utaidhinishwa na Bunge la Kitaifa. Kisheria, ODM ndiyo inastahili kushikilia nyadhifa hizo kwa kuwa ndicho chama kilichoshinda viti vingi baada ya UDA anayoiongoza Rais Ruto. Mnamo Jumatano, Rais Ruto aliwateua Bw Mbadi ambaye pia ni mwenyekiti wa ODM kama Waziri wa Fedha, Bw Wandayi (Kawi na Mafuta), Gavana wa zamani wa Kakamega Wycliffe Oparanya (Vyama vya Ushirika) na Gavana wa zamani wa Mombasa Hassan Joho (Madini na Uchumi Baharini). Bw Joho na Bw Oparanya wote ni manaibu viongozi wa ODM naye Bw Mbadi ni mwenyekiti huku Bw Wandayi akiwa kiongozi wa masuala ya kisiasa na kiongozi wa wachache bungeni. Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna mnamo Jumatano asubuhi alisisitiza kuwa wanne hao walijiunga na utawala wa Kenya Kwanza kama watu binafsi. “Je tuliwajua watu ambao tulikuwa tunazungumza nao, ndio. Ni jambo ambalo lilifuata sheria za chama, la. Tuliidhinisha hatua ya wanne hao kujiunga na serikali, hapana. Kwa hivyo, huu si uamuzi wa ODM,” akasema Bw Sifuna. “Natarajia kuwa kabla hawajaenda kuhojiwa na Bunge, watatuma barua za kujiondoa kwenye nyadhifa wanazoshikilia. Matarajio yangu ni hayo kwa sababu hawawezi kujiunga na baraza la mawaziri kama wanachama wa ODM na pia bado wana vyeo ndani ya chama,” akaongeza Bw Sifuna. Hata hivyo, Seneta wa Kisumu Tom Ojienda amesema ni jambo lisilowezekana kwa wanasiasa hao wanne kujiunga na mrengo wa Dkt Ruto bila idhini ya Bw Odinga. “Mbadi, Joho, Oparanya na Wandayi hawawezi kuteuliwa kwenye baraza la mawaziri na Rais Ruto bila baraka za Raila. Watahitajika wajiuzulu kwenye nyadhifa zao ndani ya bunge na kwa chama cha ODM,” akasema Bw Ojienda.

Support Our Website

Ads help us keep our content on kenyalivetv.co.ke free for you. Please consider supporting us by disabling your ad blocker or whitelisting our site in your ad blocker settings.

You are currently offline.
You are back online.